Simu Chanzo cha Maendeleo, Ndoa Nyingi Kusambaratika

 AJIRA ZA UHAKIKA NJE NJE, BONYEZA HAPA

Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili katika mikoa mbalimbali nchini umegundua kuwa mbali ya kusambaratisha ndoa nyingi, simu pia zimekuwa adui mkubwa kwa baadhi ya watumiaji badala ya kuwanufaisha kama inavyotakiwa.
Uzuri na ubaya wa simu
Wananchi walieleza uzuri na ubaya wa simu ambapo Peter Tesha mkazi wa Arusha aliitaja simu kuwa ndiyo chanzo cha kumfikisha alipo sasa akikosa fedha za matumizi yake ya kawaida licha ya awali kumiliki miradi mingi iliyokuwa ikimwingizia kipato.
Anaeleza kuwa baada ya kuoa mwaka 2009, alibahatika kupata watoto wawili na mkewe na maisha yao yakaendelea vizuri huku yeye akiendelea na biashara yake ya maduka matatu aliyokuwa akilimiki jijini Arusha na mawili ya Moshi.
Anasema kuwa katika maisha yake na mkewe hakuwahi kushika simu ya mkewe huyo mbali mkewe kuwa hodari wa kuchunguza simu yake.
Hata hivyo siku moja bila kupanga alichukua simu ya mkewe na kusoma ujumbe mfupi aliotumiwa, jambo analoapa kutolifanya tena maishani mwake kwani alikutana na ujumbe aliouelezea kuwa ulikuwa wa majibizano kati ya mkewe na mwanamume mwingine ambaye hata hivyo jina lililotumika lilikuwa la kijiji badala ya mtu.
“Siwezi kusahau, hata huu umaskini unaoniandama ni madhara ya simu. Ujumbe ule ulikuwa wa kulaumiana kati ya mke wangu na huyo mwanamume kuwa hawa watoto wangu ni wake, mke wangu akiuliza; Kwa nini umewatelekeza na kuniachia mzigo wa kulea mimi ambaye siyo watoto wangu?”anasema Tesha.
Anafafanua kuwa ujumbe huo ulifafanua: “Kama akiendelea kufanya hivyo ataiuzilia mbali nyumba aliyompa kwa ajili ya watoto, ambao mimi siku zote nilikuwa nikiamini ni baba yao.”
Anaeleza kuwa tangu alipofungua simu ya mkewe na kusoma ujumbe huo maisha yake yalibadilika kwani alikwenda kuwapima DNA watoto hao na kumbana mama yao ambapo ilibainika kuwa ni kweli watoto hao sio wake, jambo lililomchanganya na kumtia aibu kwenye familia na jamii hivyo akaamua kuwa mlevi.
Tesha anasema kuwa kuanzia hapo aliacha kusimamia biashara zake kutokana na kuchanganyikiwa na kukwepa aibu, huku akiishi kwa kujificha kwa zaidi ya mwaka na alipotulia na kujifikiria kwa nini amekuwa hivyo alikuwa tayari ameshachelewa, kwa kuwa baadhi ya maduka yalikuwa yamefungwa na aliowaacha hakuwa na cha kuwafanya akibaki na duka moja la Arusha ambalo pia lilikuwa limekufa kutokana na kuwa na bidhaa chache.
“Naishi kwa ushauri na ndiyo maana mara nyingi nimekuwa nakutumia ujumbe wa kutaka unishauri kwa kuwa siiamini tena akili yangu wala mwili wangu. Kama mwanamke ambaye nilikuwa naishi naye miaka yote aliweza kubeba mimba za mtu mwingine na nisijue, sina sababu ya kujiamini tena, nimekuwa masikini kwa sababu ya simu, sitamani simu ya mtu zaidi ya hii yangu, ambayo wakati mwingine huwa naamua kuifunga,”anamaliza Tesha.
Wakati Tesha akieleza hayo, upande mwingine Jennipher Lazaro wa Tanga anasema kuwa hawezi kuishi bila simu kwa kuwa humsaidia mambo mengi ikiwamo kujifunza zaidi kupitia mtandao, kumuunganisha na marafiki walio mbali naye.

Anafafanua kuwa akiambiwa achague kati ya simu na kuzungumza na mtu anayempenda kama mumewe atachagua simu kwa kuwa haimuuzi, lakini mumewe kuna siku huwa anamkera.
Naye Zaituni Mapunda (siyo jina halisi) wa Mbeya anasema kuwa simu kwake ni rafiki na adui, kwani imekuwa ikimpa mambo mengi mazuri huku pia ikimsababishia matatizo.
“Nikiachwa basi, cha kwanza kukilaumu ni simu kwani mara nyingi nakorofishana na mpenzi wangu, anakuta ujumbe niliotumiwa na wanaume wengine nasahau kuufuta,”anasema Mapunda.
Anafafanua kuwa mbali na hayo, bado anaithamini zaidi simu kwa kuwa ni kiunganishi kikubwa kati yake na watu wake wa karibu, huku akikiri kuwa mara nyingine hufanyia mambo yasiyo sahihi, ikiwemo kuwasiliana na wanaume wengi kwa wakati mmoja, ambao huwapanga kirahisi kwa kutumia simu.
“Nina uwezo wa kuwa na wanaume wengi kwa kutumia simu, lakini pia maisha yangu yanakuwa na unafuu kupitia simu,”anasema na kuongeza:
“Kama nitapewa adhabu kubwa basi ni kuambiwa nisiwe na simu au mpenzi wangu akishinda na simu yangu hawezi kuishi wala kunipenda tena maishani mwake, kwani atapigiwa simu na wenzake hadi atashangaa.”
Mudi Mkotopaje wa Dar es Salaam anasema kuwa ameshaacha wanawake wawili kutokana na kukuta maovu kwenye simu na kwamba aliyenaye kwa miaka miwili tangu waoane hataki awe na simu.
Anafafanua kuwa simu ni kishawishi kikubwa na kwamba wanawake wote aliwaacha huku bado anawapenda na wote walikuwa na kesi zinazofanana za kuwa na matumizi mabaya ya simu kwa kufanya uhusiano usio rasmi.
Anatoa ushauri kuwa hata kwa wazazi ili mabinti zao wasome kwa uhuru na kuelewa walichokusudia wasipewe simu.
Mwamvua Jumbe mama wa watoto wawili, anasema kuwa aliachana na mumewe kutokana na kumkuta na ujumbe wa mapenzi karibu kila siku.
“Wazazi wangu na wake walinikanya kuhusu kuchunguza simu yake nilishindwa kwa kuwa nilikuwa nampenda na nilikuwa naamini kuwa kuna kitu tofauti anafanya kunizunguka. Kila nilipojaribu kumchunguza nilimkuta na hatia. Kama ikitokea nikaolewa tena sintotaka kuwa karibu na simu ya mume wangu ili nisijue anachokifanya, kutokana na kupata shida ya kumlea mtoto peke yangu ,”anasema.
Mwanasaikolojia azungumza

Mtaalamu wa masuala ya saikojia wa Chuo Kikuu cha Dodoma (Udom) Modesta Kimonga alisema kuwa matumizi mabaya ya simu ni kifo kwa kuwa akili ya binadamu inabadilika kulingana na tukio lililotokea.
Alitoa mfano kuwa wakati msiba ukitokea mtu analia, akiona kitu siyo cha kawaida anaweza kufurahi au akatabasamu, akiongeza kuwa mtu ikiona kitu tofauti na inavyotarajiwa hubadilika na ndiyo sababu kuna watu wanajiua kwa vitu vidogo.
“Miongoni mwa vitu ambavyo tunatakiwa kuwa na tahadhari navyo ni simu kwani vinaweza kuleta athari kubwa kama havikutumiwa vizuri kwa matumizi yaliyokusudiwa tofauti na hapo zinaweza kuleta maafa,”anasema na kufafanua:
“Kwa mfano mume au mke anapekua simu ya mmojawao bila idhini ya mwenzake na kukuta kitu tofauti kinachoweza kumpa hasira, akapata matatizo ya kiafya au akaenda kumdhuru mkewe au mumewe kutokana na akili yake kuvurugika kutokana na alichokiona. Kila mmoja aelewe kuwa simu ya mkononi ni kwa ajili ya mwenye nayo.”
Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA)
Mtaalamu wa takwimu ya Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania, Hango Juma, alitaja idadi ya watumiaji wa simu nchini hadi Machi mwaka huu kuwa ni 27.6 milioni na kwamba mwenye haki ya kutumia simu ni mhusika wa simu hiyo.
“Si ruhusa kwa asiyekuwa mmiliki halali wa laini kuipeleleza kwa kwenda kwenye kampuni ya simu kujua amewasiliana na watu wangapi au kwa namna yoyote ile. Wafanyakazi kwenye kampuni za simu wanatakiwa kutunza siri za wateja kisheria na siyo kuzisambaza au kuzitoa kwa wahusika hata kama ni laini zao,”anasema Juma.
Tafiti yagundua
Wakati hali ikiwa hivyo Tanzania, nchi 11 za Ulaya zimefanyiwa utafiti na kubaini kuwa asilimia 94 ya watu wazima huona ni heri waishi bila ngono kuliko kuishi bila simu za mkononi, huku asilimia 65 ya watu waliofanyiwa mahojiano wakisema kuwa hawawezi kuishi bila simu na asilimia 53 walikiri kuwa wameathirika na simu zao.
Zaidi ya 2,570 watu wazima nchini Uingereza, wenye umri kati ya 18 na 30, walishiriki katika utafiti uliofanywa na Mobileinsurance.co.uk ambapo iligundulika kuwa asilimia tisa ya watu wazima wa Uingereza huona ni heri kuishi bila watoto wao kwa wiki kuliko kukaa bila simu za mkononi.
-------------------

NAFASI ZA AJIRA 

JIUNGE NA AJIRA YAKO TELEGRAM GROUP HAPA

INTERNSHIP VACANCIES

GOVERNMENT VACANCIES

NGO'S VACANCIES 

GOODLUCK

Tags

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad