RIPOTI YA MAUAJI YA ARUSHA YAVUJA....

 AJIRA ZA UHAKIKA NJE NJE, BONYEZA HAPA

HATIMAYE ripoti ya Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, kuhusu vitendo vya uvunjaji wa haki za binadamu na mauaji yaliyotokea Arusha Januari 5, 2011 kwenye maandamano ya CHADEMA imevuja.

Licha ya ripoti hiyo kufichwa kwa kutosomwa hadharani kwenye vyombo vya habari kutokana na kulishutumu moja kwa moja Jeshi la Polisi, Tanzania Daima imefanikiwa kuinasa.

Maandamano hayo ya CHADEMA ya kupinga ukiukwaji wa kanuni na sheria katika uchaguzi wa Meya ya Manispaa ya Arusha, Gaudence Lyimo, licha ya kuruhusiwa na polisi awali baadaye yalipigwa marufuku na Mkuu wa Jeshi hilo nchini, IGP Saidi Mwema.

Hata hivyo, CHADEMA walikataa kutii agizo hilo kutokana na taarifa ya IGP kutowafikia kwa maandishi kama inavyoelekezwa kwa mujibu wa taratibu za utendaji wa jeshi hilo.

Kufuatia vurugu hizo za polisi na wafuasi wa CHADEMA, watu watatu waliuawa kwa kupigwa risasi, wengine zaidi yya 30 kujeruhiwa na wafuasi zaidi ya 70 wakiwemo viongozi waandamizi wa chama ambao walifunguliwa mashtaka mahakamani.

Kutokana na tukio hilo Tume ya Haki za Binadamu, iliunda tume iliyochunguza suala hilo Januari 10 hadi 13 mwaka 2011, kwa kuwahoji viongozi wa CHADEMA mkoa wa Arusha, Jeshi la Polisi, hospitalini walipolazwa majeruhi na njiani walipoandamana wafuasi wa chama hicho.

Tume hiyo iliongozwa na Kamishna Joaquine De-Mello akiandamana na ofisa uchunguzi, Philipo Sungu, kutoka idara ya elimu kwa umma na mafunzo kufuatilia tukio hilo kwa muda wa siku tatu ili kupata picha halisi.

Lengo kuu lilikuwa kubaini chanzo cha vurugu hiyo, uvunjwaji wa haki za binadamu ambapo Januari 11, asubuhi tume hiyo ilianza kuonana na madaktari na wagonjwa majeruhi waliolazwa katika hospitali mbili za Mount Meru na Seliani.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo ambayo gazeti hili linayo nakala yake, taarifa zilizopatikana katika hospitali zilionyesha kupokelewa kwa majeruhi 26 katika hospitali ya Mount Meru na wawili Seliani.

Majeruhi watatu walipoteza maisha wakati wakipatiwa matibabu ya awali hapo hospitali ya Mount Meru, 22 walilazwa katika hospitali ya Mount Meru na watatu walipatiwa matibabu na kuruhusiwa kuondoka hospitalini.

Ripoti ya madaktari ilithibitisha kuwa vifo hivyo vilitokana na majeraha ya risasi za moto huku majeruhi wengine wakithibitisha kupigwa risasi za moto huku wakionyesha majeraha hayo kwenye miili yao.

Licha ya ripoti kuonyesha vitendo hivyo vya uvunjifu wa haki za binadamu uliofanywa na polisi, inasema kuwa maandamano ya CHADEMA na mkutano yalikuwa halali na jeshi ndilo lilisababisha fujo hizo kwa kutofuata sheria.

“Tanzania inajivunia Katiba inayoainisha vipengele mbalimbali vinavyotambua na kulinda haki za msingi za binadamu, hivyo kama nchi nyingine inawajibika kwa Azimio la Ulimwengu la Haki za Binadamu la mwaka 1948 (UDHR) ambalo ni mama wa matamko, makubaliano na mikataba ya vizazi vyote vya haki,” inasema ripoti hiyo.

Kwamba Tanzania kama miongoni mwa nchi wanachama zilizoweka sahihi na kuridhia mikataba hiyo zinawajibika moja kwa moja “kuheshimu, kulinda, kutetea na kutekeleza” haki zilizoainishwa kwenye mikataba husika.

Ripoti hiyo inaongeza kuwa “kanuni za jumla za jeshi la polisi namba 403 kifungu cha kwanza inasema; Mtu yeyote ambaye anataka kuitisha, kukusanya, kuandaa na mkutano wowote au maandamano katika eneo lolote hadharani atapaswa kuwasilisha taarifa ya maandishi si chini ya saa 48 kabla ya wakati mkutano au maandamano kufanyika kwa ofisa wa polisi wa wilaya husika.

Na pindi anapopelekea taarifa kwa maandishi kwa mkuu wa polisi wa wilaya anaruhusiwa kuendelea kuandaa, kuitisha, kukusanya, kuunda, au kuandaa mkutano au maandamano kama ilivyopangwa.

Ila mpaka atakapopata taarifa ya maandishi kutoka kwa Afisa Polisi wa Wilaya husika kueleza sababu za kusitisha maandamano hayo.”

Ripoti hiyo inasema kuwa kwa mujibu wa sheria hiyo, polisi “Officer in charge” wa eneo katika eneo hilo la Arusha mjini ni OCD wa Arusha Mjini – ndiye aliyepaswa kutoa maelekezo ya kuzuia maandamano na si Kamanda wa Polisi wa Mkoa au Inspekta Jenerali wa Polisi.

“Kwa mantiki hii, taarifa ya CHADEMA kwa polisi ilitosha kwa wao kuendelea na mipango yao ya maandamano na mkutano kama inavyoelezwa kisheria,” anasomeka taarifa hiyo.

Pia inaonyesha kuwa Sheria Na. tano (5) ya mwaka 1992 ya vyama vya siasa kifungu cha 11 vifungu vidogo vya (4) na (6) na sheria Na. 1 ya 1939 ya polisi na huduma za mgambo kifungu 43.-(1), (2), zilikidhi pia hitaji la CHADEMA kuendelea na mipango yao ya maandamano na mkutano wa hadhara kama ilivyopangwa.

Kwamba Sheria Na.5, 1992 ya vyama vya siasa kifungu 11. — (8) inasema: kama jeshi la polisi linasitisha maandamano au mkutano taarifa hizo hutolewa kwa maandishi kueleza sababu, wala si kutumia televisheni, kama ilivyojitokeza kwa tukio la Arusha.

“Hivyo CHADEMA walikuwa sahihi kwa kuwa hawakupata taarifa ya kimaandishi licha ya polisi kudai kutoa barua hiyo lakini walishindwa kuthibitisha madai yao mbele ya tume.

Ripoti hiyo pia inaongeza kuwa askari walifanya vitendo vya unyanyasaji na udhalilishaji dhidi ya viongozi na waandamanaji hasa wanawake bila kujali hali zao.

Kwa mfano wanatajwa mbunge wa viti maalum Lucy Owenya na mke wa Katibu Mkuu wa CHADEMA, Josephine Mushumbusi, kuwa walipigwa na kujeruhiwa vibaya sehemu mbalimbali za miili yao.

Kwamba viongozi wa CHADEMA na wananchi wengi walikamatwa na kuwekwa rumande katika kituo kikuu cha polisi kati mjini Arusha.

“Askari waliwapiga waandishi wa habari, waliwanyang’anya vifaa vyao vya kazi na kufuta picha na kazi walizokuwa wanazifanya kwenye maandamano. Askari na waandamanaji walisababisha uharibifu wa magari na mali za umma na wananchi.

“Aidha walisababisha upotevu wa mali za wananchi zikiwemo simu mbili za mkononi za Owenya na fedha tasilimu sh 2,700,000 za majeruhi Ally Ogaga walizodai kunyang’anywa na askari, wakati Ofisi ya CCM Mkoa wa Arusha ilivunjwa vioo kwa mawe na waandamanaji na nyumba ya mwananchi Salum Ally iliungua kwa moto uliosababishwa na mlipuko wa bomu lililoruka kutoka kwenye gari la polisi,” ilisomeka.

Tanzania Daima
-------------------

NAFASI ZA AJIRA 

JIUNGE NA AJIRA YAKO TELEGRAM GROUP HAPA

INTERNSHIP VACANCIES

GOVERNMENT VACANCIES

NGO'S VACANCIES 

GOODLUCK

Tags

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad