google-site-verification: googleb0bc30c3e5fdb812.html Pinda: UKAWA Njooni Tuombane Msamaha | UDAKU SPECIAL

Pinda: UKAWA Njooni Tuombane Msamaha

 AJIRA ZA UHAKIKA NJE NJE, BONYEZA HAPA

Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, ‘amewaangukia’ wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba wanaounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) kutoendelea na msimamo wao, badala yake wakutane ili atakayebainika kuteleza na kusababisha mgogoro waombane radhi na kuendelea mchakato wa kupata katiba mpya.

Pinda alisema hayo jana wakati akiweka jiwe la msingi katika Chuo cha Ufundi Gonja/Mheza, kilichopo Wilaya ya Same, mkoani Kilimanjaro.

“Wenzetu wanaojiita Ukawa wameamua kususia Bunge Maalumu la Katiba, lakini jitihada zinazoendelea sasa hivi ni kuwasihi warudi bungeni kwa sababu mjadala upo bungeni.
Na mimi nawasihi waje tuzungumze, tuelewane na pale tunapoonekana tuliteleza tuombane msamaha ili tusonge mbele na kupata katiba, ambayo wananchi wanaitarajia,” alisema Pinda.

Alisema hakuna haja ya kubishana katika mambo, ambayo bado waamuzi wa mwisho wa mchakato mzima wa katiba mpya watabaki kuwa ni wananchi, ambao wataamua kwa kupiga kura ya maoni baadaye mwaka huu.

“Uzuri wenyewe ni kwamba, chochote kile tutakachokubaliana pale bungeni si lazima kikakubaliwa na wananchi. Kwa sababu kule mwisho kuna kura ya maoni.
Kwa hiyo, wananchi ndiyo watakaosema hiki ndiyo na hiki sicho…Hakuna haja ya kubishana kwenye kitu, ambacho wananchi watakuwa ndiyo wenye maamuzi ya mwisho,” alisema Pinda.

Kuhusu uchaguzi wa serikali za mitaa unaotarajiwa kufanyika Oktoba, mwaka huu, Pinda alisema serikali itatumia katiba ya sasa katika uchaguzi huo endapo Ukawa wataendelea kushikilia msimamo wao wa kutorudi bungeni au kuafikiana.

Alisema iwapo Ukawa hawatarudi bungeni mwezi ujao, katiba ya sasa (ya mwaka 1977) itaendelea kutumika ingawa italazimika kufanyiwa marekebisho katika maeneo Fulani, ambayo hakuyataja baada ya maridhiano na pande zote.

UKAWA, CCM wakwama
JK akingiwa kifua asikutane na wajumbe
Kinana na timu yake waja na ajenda mpya
Katibu Mkuu wa CCM, KinanaMAZUNGUMZO yanayoendelea kuhusu jinsi ya kunasua mchakato wa katiba mpya kati ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na wajumbe wanaounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA), yanaelekea kukwama kwa sababu yameingiliwa na hila, Tanzania Daima Jumatano limebaini.

Kwa mujibu wa vyanzo vyetu vya taarifa, kikao cha mwisho kilivunjika bila muafaka kutokana na CCM kuleta mapendekezo yasiyotekelezeka, kama njia ya kuondoa wajumbe kwenye hoja kuu.

Miongoni mwa mapendekezo mapya yaliyoletwa mezani, ni pamoja na kutaka wajumbe wajadili maeneo mengine ya sheria ambayo CCM haiyataki, na kutaka wajumbe wengine waongezwe katika mjadala huo ili idadi iwe kubwa zaidi.

Hata hivyo, kwa mujibu wa taarifa tulizonazo, wajumbe wa UKAWA walikataa mapendekezo hayo kwa misingi kwamba hoja ya kwanza ingesababisha warudi kwenye hoja nyingine inayohoji jinsi Rais Jakaya Kikwete alivyoteua baadhi ya wajumbe wa kundi la 201, ambao imekuwa inadaiwa kwamba wengi wao ni mawakala wa CCM walioongezwa makusudi ili kukuza idadi kwa ajili ya kuongeza kura katika hatua ya uamuzi.

“Katibu Mkuu wa CCM alipoleta hoja hiyo, wenzetu wakamwonyesha kwamba kupanua maeneo yenye ugomvi ni kufungua Pandora box ambalo CCM tusingelipenda, kwa mfano kuanza kuhoji upya idadi na utaratibu wa kupata wajumbe wa kundi la 201. Hoja hiyo ikafa,” kilisema chanzo chetu kilicho karibu na kiongozi huyo.

“Ndipo alipopendekeza kuwa ingekuwa vema waletwe wajumbe wengine kwenye mazungumzo, ambao ni wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba, hoja ikapingwa pia na wajumbe wa UKAWA kwa maelezo hao ni sehemu ya waliosababisha mazungumzo kuvunjika.”

Chanzo chetu kiliongeza: “UKAWA walisema kwamba hao ndio waliokimbiwa bungeni, na kwamba kuwaleta kwenye mjadala kungesababisha mabishano zaidi badala ya kutafuta usuluhishi.

“Mjumbe mmoja alizungumza kwa ukali, kwamba hiyo ni non-starter, kwamba UKAWA wametoka kwa sababu ya wajumbe hao hao, hivyo kuwaleta kwenye mazungumzo haya kungekuwa sawa na kuongeza watu walewale halafu kutarajia matokeo tofauti.”

Kwa mantiki hiyo, mjumbe mmoja aliyeshiriki mjadala huo, huku akikataa kuingia kwa undani, amekiri kwa kusema kwamba “mazungumzo hayaendi kokote.”

Hata hivyo, baada ya Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana na timu yake kukataliwa mapendekezo yao mawili kwa sababu hizo, wajumbe wa UKAWA walitoa pendekezo jipya, ambalo kwa ujumbe wa CCM lilionekana kuwa zito na gumu zaidi.

“Walipomaliza kupangua mapendekezo yetu, ndipo nao wakapendekeza kwamba badala ya watu walewale, sasa ni vema waitwe marais wawili – Jakaya Kikwete wa Muungano na Dk. Ali Mohamed Shein wa Zanzibar, ambao ndio viongozi wa mihimili ya dola,” alisema mtoa habari huyo na kuongeza:

“Nani akubali? Hapo katibu mkuu (Kinana) na timu yake waliruka kama wameona joka kubwa, kwa sababu tunajua rais akikutana na wapinzani anaweza kuwasikiliza. Imeshatokea huko nyuma, na hatutaki itokee sasa, maana rais akishakubali hoja zao, kama chama tutalazimika kufuata ushauri atakaotoa, nao watakuwa wameshinda.”

Hoja ya UKAWA kutaka kujadiliana na marais wawili ililenga kumpa fursa Rais Kikwete kurejesha nyuma msimamo wake kuhusu rasimu ya pili ya katiba, maana siku alipozindua Bunge la Katiba, aliweka msimamo ambao ndio umekuwa ukifuatwa na wajumbe wote wenye maslahi na CCM.

Mara kadhaa, baadhi ya watu mashuhuri na taasisi zimesema kwamba kama Rais Kikwete asingeleta msimamo wa chama chake bungeni, ingejadiliwa rasimu ya tume, na UKAWA wasingetoka.

Miongoni mwa watu maarufu waliokiri kwamba rais alikosea ni pamoja na Msajili ya Vyama vya Siasa mstaafu, John Tendwa, ambaye alikiri kwamba rais aliteleza.

Jumuiya ya Wakristo Tanzania (CCT) ilitoa waraka wake kusisitiza hoja hiyo, kwamba kauli ya rais ndiyo ilivuruga mchakato, na kwamba ili Bunge liendelee kwa amani inabidi wajumbe wote wajielekeze kwenye rasimu ya pili ya katiba iliyowasilishwa na Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba.

Mara kadhaa, viongozi wa UKAWA wametamka wazi kwamba iwapo mjadala wa Bunge hilo hautajikita katika rasimu hiyo, hawatarejea bungeni.

Serikali imekuwa inafanya jitihada za chini chini, na za wazi kuhakikisha wajumbe wa UKAWA wanarudi bungeni, lakini wao wanadai kwamba hawawezi kurudi kujadili rasimu ya CCM badala ya rasimu ya wananchi iliyowasilishwa na Jaji Warioba.
-------------------

NAFASI ZA AJIRA 

JIUNGE NA AJIRA YAKO TELEGRAM GROUP HAPA

INTERNSHIP VACANCIES

GOVERNMENT VACANCIES

NGO'S VACANCIES 

GOODLUCK

Post a Comment

2 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.
  1. Hiyo picha inatisha.wadau.nitaota.ni ya homo sapiens na homo habilis?

    ReplyDelete
  2. Admn habari ndefu mno inachosha....

    ReplyDelete

Top Post Ad