MAPYA: Waajiri Waanza Kuwafukuza Madereva Waliogoma......CHAKUA, UWAMATA,CHAMAMATA Watoa Matamko

 AJIRA ZA UHAKIKA NJE NJE, BONYEZA HAPA

BAADHI ya madereva waliogoma katika mgomo wa juzi uliodumu kwa siku mbili wameanza kufukuzwa kazi na wamiliki wa mabasi hayo.

Mhasibu Mkuu wa Umoja wa Madereva Tanzania(UWAMATA) Issa Regan aliwataka matajiri kuwarudisha kazini dereva huyo na kama hawatawarudisha watawaambia madereva wote wa kampuni hiyo kugoma.

Regan aliongeza kuwa makosa sio ya madereva hao kwa kuwa walitii umoja huo na viongozi wao ndio waliwaambia kugoma hivyo kumfuza dereva sio sawa.

“Nasikitika kwa kitendo hicho na kama hawa matajiri wanataka vita basi tupo radhi kufanya hivyo lakini sisi tunataka kujenga mahusiano mazuri kati ya madereva na mabosi wao suala letu lilikuwa ni suala la msingi mtu ashindwe kuelewa mi sijui wanatutaka nini” alisema Regani.

Alimtaja dereva aliyefukuzwa na mmiliki wake kuwa ni Seif Kitumbo wa basi la kwenda Musoma, ambaye ni wa kampuni ya Osaka.

Regan alieleza kuwa wameshatoa taarifa kwenye vyombo vya  usalama kuwa endapo akipotea kiongozi yeyote wa chama chetu cha madereva bila mawasiliano (kutekwa) sisi tutashughulika na matajiri.

Naye dereva aliyefukuzwa katika gari hilo kwa sababu ya mgomo, Kitumbo alisema kuwa chanzo cha yeye kufukuzwa ni kwa sababu aligoma na tajiri wake alimwambia kuwa amemsababishia hasara.

“Nimekuja kwenye chama chetu hiki ili niweze kusaidiwa nimefanya kazi kwa muda wa mwaka mmoja na miezi 11 sijawahi kusababisha ajali yoyote”alisema Kitumbo.

Naye Katibu Mkuu wa UWAMATA,Abdala Lubala alisema athari za kutoajiriwa ndizo hizo kama Kitumbo angekuwa anamkataba asingefukuzwa kirahisi kama hivyo.

“Wamiliki wanatutafuta sisi tuligoma kwa haki yetu madereva tutafata sheria za kuweza kumsaidia huyu dereva arudishwe kazini lakini dunia imekubali madai yetu kuwa ni ya msingi”alisema Lubala.

Amri  ya  Kurudi  Shule  Yafutwa
Akizungumza na waandishi wa habari jana kituoni hapo, Katibu wa Umoja huo Abdul Lubanda alisema kero moja kati ya madai yao tayari limefanyiwa kazi na Serikali.

Alisema kero hiyo ni ile ya madereva kurudi shule kusoma kila baada ya miaka mitatu ambayo walikuwa wakiipinga.

“Baada ya kikao cha jana (juzi)tuliondoka na Mkuu wa Wilaya, Paul Makonda hadi kwa Waziri Mkuu kwa ajili ya kushughulikia masuala ambayo tulikuwa tunayalalamikia pamoja na kujua tume iliyoundwa.

“Tulikuwa pia na Waziri wa Uchukuzi, Samuel Sitta tulikuta tayari kero ya kurudi shule imeondolewa kimaandishi kama ambavyo tuliomba,” alisema.

Alisema walielezwa muundo wa tume (kamati) iliyoundwa na Waziri Mkuu Mizengo Pinda kwamba itajumuisha makatibu wakuu wa wizara nne pamoja na taasisi mbalimbali zinazohusiana na mambo ya usafirishaji.

Alitaja Wizara hizo ni pamoja na Ujenzi, Uchukuzi, Kazi na Ajira na Miundombinu na vyama hivyo ni Chama Cha Wamiliki wa Malori (TATOA), Chama cha Wamiliki wa Mabasi (TABOA), Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (SUMATRA), Chama cha Madereva, Chama cha Kutetea Abiria (CHAKUA).

 Alisema kamati hiyo itakuwa ikikutana mara moja kila mwezi na kwamba ital;azimika kukutana mara kwa mara iwapo kuna tatizo kama lililojitokeza hivi sasa la mgomo ili kulipatia ufumbuzi.

“Chama cha Madereva tumepatiwa nafasi tano za wajumbe ndani ya kamati hiyo leo (jana) tumekuwatana ili kuwateua wawakilishi wetu, kamati itakapoanza kazi  itashughulikia suala la mikataba ndani ya siku 30, tunataka kila dereva apatiwe mkataba bora na si bora mkataba na mwajiri wake,” alisema.

Alisema kutokana na mgomo uliomalizika wanaimani kwamba kilio chao kimewafikia wahusika na kwamba kamati hiyo itasimamia kwa weledi ili kuendelea kutatua changamoto zilizokuwa zikiwakabili.

Hali  ya  Kituo
Meneja wa kituo hicho, Juma Idd alisema idadi kubwa ya watu waliokuwa ndani ya kituo hicho kipindi chote cha mgomo iliwapa changamoto kubwa.

“Watu walikuwa wengi kupita kawaida, kwa sababu wengi ni wageni hawajui kama hapa kituoni tuna majengo matano ya vyoo ambayo yanajumla ya matundu…. Ilibidi tuwaelekeze watu sehemu hizo,” alisema.

Idd alisema anamshukuru Mungu kwamba licha ya mgomo huo kuwepo kwa takriban siku mbili, huduma ya maji ilikuwepo katika kipindi chote na hivyo vyoo hivyo kufanyiwa usafi kila mara kwani hali ingeweza kuwa mbaya zaidi.

Akizungumzia juu ya kupanda kwa gharama za vyakula kituoni hapo alisema Halmashauri haihusiki na jambo hilo kwani huduma hiyo hutolewa na watu binafsi.

“Watu walikuwa wakilalamika kupanda kwa gharama za chakula, kuna msemo wanasema kufa kufaana pengine wapo baadhi ya wafanyabiashara ambao waliona watumie mwanya huo kujipatia faida na labda kwa sababu bidhaa zilikuwa hazipelekwi sokoni ikapelekea kupanda kwa gharama za manunuzi,” alisema.

CHAKUA watoa  Wito
Katibu Msaidizi wa Chama cha Kutetea Abiria (Chakua) Godwin Ntongeji alitoa wito kwa wamiliki wa mabasi kutochukua nauli kwa abiria iwapo wanajua madereva wao watafanya mgomo.

Aliwataka wamiliki hao kufunga kabisa vituo vyao ili abiria wasikate tiketi kuliko kuwasababishia usumbufu kama huo walioupata kituoni hapo katika kipindi hicho cha mgomo.
 
“Vyakula vilipanda bei, wengine walikuwa wanakwenda msibani ikashindikana, na  kuna mwanamke mmoja alikuwa mjamzito akapatwa na uchungu ghafla usiku ilibidi wanawake wenzake wamsaidia walikwenda naye pembeni wakamzingira, wakamzalisha kisha akakimbizwa hospitalini,” alisema.

Chama cha Madereva  wa  Maroli
Mwenyekiti wa Chama cha Madereva wa Maroli (Chamamata), Clement Masanja, alisema watawashtaki wamiliki wote ambao watawafukuza madereva wao.

Alisema kitendo cha wamiliki kuanza kuwafukuza madereva ni cha uonevu kwani walikuwa wanadai haki zao za msingi.
 
“Tutafuatilia kujua kama huyo dereva aliyefukuzwa aliajiriwa kwa mkataba na kama hakuwa nao sisi kama chama tunao uwezo wa kumshtaki,” alisema Masanja.
-------------------

NAFASI ZA AJIRA 

JIUNGE NA AJIRA YAKO TELEGRAM GROUP HAPA

INTERNSHIP VACANCIES

GOVERNMENT VACANCIES

NGO'S VACANCIES 

GOODLUCK

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad