Lowassa: Miaka 50 ya Kuteswa na CCM Imetosha......Watanzania Msiogope Kufanya Mabadiliko

 AJIRA ZA UHAKIKA NJE NJE, BONYEZA HAPA

Lowassa Akihojiwa na Waandishi wa Habari
Mgombea urais wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Edward Lowassa, amesema mwaka huu ni wa mabadiliko ili kuiokoa nchi na madeni mengi ambayo yanasababisha uchumi kuyumba.

Lowassa ambaye ameambatana na Waziri Mkuu wa mstaafu wa awamu ya tatu, Frederick Sumaye, aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani, Laurence Masha, aliyekuwa Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Shinyanga, Khamis Mgeja na viongozi wengine, walianza ziara yao ya kampeni za kuomba kura kwa wananchi Jumatatu wiki hii.

Ziara ya mgombea urais huyo zilianzia Mkoa wa Iringa ambako alizungumza na maelfu ya wananchi kwenye mikutano ya hadhara katika majimbo ya Kilolo, Mufindi na Iringa mjini na jana (Jumanne) aliwasili katika Mkoa wa Njombe na kuzungumza na wananchi wa majimbo ya Makambako na Njombe mjini.

Akizungumzia deni la taifa, Lowassa alisema atakapoingia madarakani atakuwa na kazi ya kulipa madeni yaliyolimbikizwa ambayo hata haijulikani yametokana na nini.

Alisema Rais Benjamini Mkapa alipoingia madarakani alipunguza deni alilolikuta likawa chini ya Sh. trilioni 10 lakini leo zimefikia zaidi ya Sh. trilioni 35.

“Kwa hiyo anayeingia madarakani itabidi aanze kutumia zile fedha ambazo zingetumika kwa ajili ya maendeleo ya Watanzania kulipa madeni. Deni la taifa ni kubwa na hizo fedha tunazodaiwa tujiulize zimefanya nini na ziko wapi,” alisema.

Alisema CCM wameanza kufilisika kutokana na kueneza taarifa zisizokuwa za kweli kwamba Chadema haina ilani wakati ilani hiyo ilizinduliwa mapema mwishoni mwa wiki iliyopita.

“CCM wana macho lakini hawaoni, wana masikio hawasikii, tumetengeneza ilani kiboko ambayo ndani ya miaka mitano nchi itapaa kimaendeleo,”alisema.

Alisema wananchi wasitishwe na propaganda kwamba wakichagua upinzani damu itamwagika na nchi itaingia katika vita kwani hakuna Mtanzania atakayemwaga damu na kwamba nchi itakuwa tulivu labda wao ndio waivuruge.

Kuhusu mgogoro kati ya wafanyabishara na TRA kuhusiana na mashine za EFD, alisema kama atapewa ridhaa na wananchi na kufanikiwa kuingia Ikulu atalishughulikia haraka suala hilo.

Kuhusu michango, michango yote isiyokuwa ya msingi katika shule za sekondari ataifuta hasa ikizingatia kuwa ilani ya uchaguzi ya Chadema imeeleza bayana kwamba elimu itakuwa bure kwa sababu fedha zipo.

Alisema atahakikisha analinda maslahi ya wafanyakazi wakiwamo walimu ambao wamekuwa wakidai madeni yao bila mafanikio.

Aliongeza kuwa miaka 50 ya utawala wa CCM imetosha na kuwataka watu wanaoogopa kuondoka CCM waache uoga waondoke.

“Wapo wafanyabiashara wanaogopa kwa sababu wanatishwa, nawaambia msiogope. Neno usiope limeandikwa mara 360 ndani ya Biblia,”alisema.

Kwa upande wa Sumaye wakati akimnadi Lowassa alisema mawaziri wa serikali hawawezi kupata ujasiri wa kupambana na rushwa kwa sababu mambo machafu yote yanayofanywa ndani ya serikali yao wanayafahamu.

Alisema mawaziri waliopo katika serikali ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), wasiwadanganye Watanzania kwamba wanaweza kupambana na rushwa kwa sababu hawana dhamira ya kweli kwani mambo mengi machafu yanayofanyika ndani ya serikali wanayafahamu. 

“Leo Magufuli (mgombea urais CCM) anasimama na kusema akiingia Ikulu atapambana na rushwa hivi yeye yupo wapi si sehemu ya serikali na ameshindwa kufanya hivyo, amekuwa waziri kwa miaka mingi hakuweza leo hii akiingia Ikulu ataweza wapi,”alisema.

Katika hatua nyingine, umetolewa ufafanuzi kuhusiana na taarifa iliyoeleza kimakosa kuwa mgombea urais wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Edward Lowassa, atafuta Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) pindi akiingia madarakani na kuligeuza kuwa la kutoa mafunzo ya ufundi stadi na kufundisha uzalendo kwa vijana.

Usahihi ni kwamba katika mkutano wake wa kampeni mkoani Iringa juzi, Lowassa aliahidi kuingiza mafunzo ya ufundi stadi kwa vijana wanaojiunga JKT ambako pia wataendelea kufundishwa uzalendo ili waje kulitumikia vizuri taifa lao; na siyo kufuta JKT.
-------------------

NAFASI ZA AJIRA 

JIUNGE NA AJIRA YAKO TELEGRAM GROUP HAPA

INTERNSHIP VACANCIES

GOVERNMENT VACANCIES

NGO'S VACANCIES 

GOODLUCK

Top Post Ad