Wazazi na Jamii, Tusiwanyang'anye Watoto Utoto Wao

 AJIRA ZA UHAKIKA NJE NJE, BONYEZA HAPA

Habarini….

Katika hatua za ukuaji wa binadamu, utoto ni hatua ya mwanzo kabisa na ya muhimu katika kipindi cha uhai wa binadamu. Katika utoto wa binadamu ndipo inapojengwa misingi ya namna gani mtu huyo atakuja kuwa akiwa kijana, mtu mzima na hata uzeeni. Japokuwa ni lazima tukiri kuwa katika kila hatua ya ukuaji wa mwanadamu kuna vitu ambavyo vinaweza kuathiri mustakabali wa mtu husika lakini hii haiondoi ukweli wa kuwa utoto ndiyo hatua ya msingi kabisa na yenye nguvu kubwa katika maisha yanayobaki kwa mwanadamu. Katika umri wa utoto ndipo picha halisi ya maisha ya mwanadamu huonekana na ndicho kipindi mwanadamu huwa na fikra zisizongwazongwa na makuu ya dunia. Ni kipindi ambacho binadamu huishi katika amnani yakweli, upendo wa kweli n.k.

Kwa kipindi kirefu sana kundi hili la watoto limekuwa likipitiwa na changamoto nyingi ambazo baadaye huja kuwa na madhara makubwa kwa wahusika wenyewe na kwa jamii iliyowazunguka. Madhara haya yanatokana na jamii au wazazi kufanya vitu vya namna Fulani ambavyo viliathiri saikolojia wakati wa utoto wao na kusababisha madhara wakati wa utu uzima wao.

Mara nyingi tunapoongelea suala la changamoto zinazowakumba watoto ambazo kwa namna moja ama nyingine huathiri maisha yao katika utu uzima wao, huwa tunawaongelea wale watoto ambao kwa namna moja au nyingine hawajapita katika maeneo sahihi wakati wa makuzi yao kama vile; watoto yatima ambao wanaishi katika mazingira yasiyo rafiki, watoto ambao migogoro ya kifamilia hasa wazazi wao imechangia wao kutokuwa na mwelekeo mwema, watoto ambao kutokana na sababu mbalimbali wamejikuta wakiishi na wazazi wa kambo ambapo wamekuwa wakinyanyaswa na wazazi hao wa kambo, watoto ambao wamezaliwa katika nchi au jamii zenye migogoro ya muda mrefu kama vile vita ambapo baadhi yao huanza kushika/kushikishwa mitutu ya bunduki katika umri mdogo kabisa.

Haya ndiyo makundi ambayo mara nyingi huwa tunayajadili na kusahau kuwa kuna kundi moja ambalo kwa macho ya nje linaonekana ni kundi ambalo liko salama zaidi na hata watoto wengine hutamani kama wangekuwa wamoja wao, bila kujua kuwa kundi hili kama lipoangaliwa kwa ukaribu laweza kuwa kundi lenye madhara mabaya sana kwa watoto. Kundi hili ni la watoto waishio na wazazi wao na kutimiziwa kila hitaji la mioyo yao.

Kwanza napenda niseme tu kuwa mimi sina mtoto na sina mpango wa kuwa na mtoto hivi karibuni, lakini hii haininyimi haki ya kuhoji ukamilifu wa malezi yatolewayo kwa watoto. Iko hivi; wazazi wengi sana wa sasa (hasa vijana) wamekuwa wakionyesha upendo mkubwa sana kwa watoto wao katika namna ya kipekee na yenye kushangaza.

Ni jambo jema sana kumpenda mtoto wako kwa sababu kwa njia hiyo utamjengea hali nzuri ya kiakili na kuishi maisha yenye mafanikio baadaye. Lakini kwa namna Fulani upendo huu umekuwa ukitolewa kwa pupa au kwa namna Fulani ambayo inaonyesha dalili kuwa endapo mambo hayatabadilika, basi jamii yetu miaka 30 ijayo itakuwa ni watu wa ajabu na wa hovyo sana. Upendo wanaopewa watoto wa siku hizi ni aina ya upendo ambao unawanyang’anya na kuitupilia mbali ile haki yao ya kuwa watoto.

Watoto wengi wa siku hizi wamekuwa wakiishi katika kivuli cha utoto lakini uhalisia hawastahili kuishi maisha hayo lakini cha kusikitisha ni kuwa, kwa kuwa hawana utashi huru wanaishi maisha hayo kwa furaha tele na akili yao ikijijenga kuwa ndiyo maisha sahihi lakini hayo ndiyo yatakayokuja kuleta vitu vya ajabu huko mbeleni.


BADO NI WADOGO, TUSIWAKUZE...

Huwa nasikitika sana ninapopita na kukutana na watoto wa miaka chini ya nane wakichambana (tofautisha ugomvi wa watoto na kuchambana), au kukuta watoto wamekusanyika wananacheza kisingeli huku wakijaribu kutikisa nyama zao ndogo kuwaiga watu Fulani Fulani ambao huwa wanapita nje ya nyumba zao kila baada ya siku kadhaa. Huwa nawaangalia na kusema kuwa sio kosa lao hata kidogo. Ni kosa la sisi wazazi na sisi wanajamii kujijali sisi na starehe zetu zisizo na msingi na kusahau kuwa kuna kizazi ambacho kinatakiwa kipite katika njia sahihi ili kije kiishi maisha yenye kupendeza.

Jamii imejawa na roho ya ubinafsi uliopitiliza, kila mtu anajijali yeye pekeyake. binti wa miaka 23 kutikisa makalio mbele ya vivulana na visichana vya miaka 8 ni ubinafsi. Matu wazima kufanya hadharani mambo ambayo yanatakiwa yafanyike wakiwa sirini ni ubinafsi. Wazazi kuangalia na watoto au filamu zenye maudhui yasiyowafaa watoto ni ubinafsi. Wazazi kuongea na waskaji au mashosti zenu mambo yasiyowajenga watoto ni ubinafsi.

Wazazi kugombana mbele ya watoto wenu ni ubinafsi. Huu ni ubinafsi wa kutokujali ni kiasi gani mtoto anaathirika kwa namna gani bila kujali hali aliyonayo wakati ule. Ubinafsi wa kudhani kuwa watoto ni viumbe huru wanaotakiwa kuishi kadri ya mapenzi yao wenyewe na kusahau kuwa sisi ndo watu wa kuwashika mikono na kuwaonyesha ni nini chafaa kwao.

Kwanini turuhusu utu uzima uanze kumea katika akili mbichi kabisa inayotakiwa kufinyangwafinyangwa ili kuifanya iwe katika umbo na mtazamo sahihi? Watoto ni kama karatasi nyeupe, kila itakachokuta nacho kwa mara ya kwanza ndicho kitakachodumu milele. Kwa nini tuwakuze wangali wabichi?


WAZAZI KUWAFANYA WATOTO MARAFIKI ZAO; ZIMWI LING’ATALO NA KUPULIZA

Wiki kadhaa hapo nyuma nilipata kusoma ‘meme’ Fulani ambayo kwa namna Fulani ilikuwa inatoa ujumbe mzito sana. Ilikuwa imeandikwa kuwa “kosa kubwa la wazazi wa sasa ni kujaribu kuwa marafiki wakubwa wa watoto wao na si kuwa wazazi ngangari”. Wazazi wengi wa siku hizi wamekuwa wakijaribu kwa nguvu sana kuwa marafiki wakubwa kwa watoto wao na kusahau kuwa wao ni wazazi na wala si washkaji au mashosti wa watoto wao.

Haimaanishi kuwa mzazi anatakiwa asiwe na ukaribu wa kirafiki na mwanae, hapana, bali ukaribu huo unatakiwa uwe na mipaka na mipaka ya msingi ni msingi wa uhusiano ulipo kuwa wao ni wazazi na hao ni watoto wao. Wazazi wamejikuta wakiwapenda sana watoto wao kiasi kwamba hawapendi kuwaona watoto wao wakiwa na hali ambayo wao kama wazazi hawapendezwi nayo bila kujua hili janga bay asana kwa hapo baadaye. Kwa mfano unaweza kuta mzazi hapendi kuona mwanae akilia, hili ni jambo zuri. Lakini unakuta anajitahidi kumfanya mtoto asilie hata katika mazingira ambayo angeweza kumfanya alie kwa muda mfupi lakini baada ya muda Fulani mtoto huyo asingeweza kulia kwa sababu hiyo tena.

Kwa kawaida watoto huvutiwa sana na vitu ambavyo watu wao wa karibu huvitumia sana, na ndiyo maana unaweza kuona ni jinsi gani watoto wa siku hizi wanapenda kuchezea simu kwa sababu wazazi wao wanatumia simu kwa muda mrefu. Sasa unaweza kuta mtoto amechukua simu na mzazi anapojaribu kuichukua ile simu mtoto anaanza kulia basi mzazi anaamua kumuachia kwa kujisemmea kuwa, atalala nitaichukua, au ataisahau muda sio mrefu nitaichukua. Zoezi hili likiwa endelevu litaanza kujijenga katika akili ya mtoto kuwa yeye ndiye yuko sahihi musa wote kwa kila akifanyalo kwa sababu anakua na ile tabia ya kuwa kila anachoklilia anaachwa awe nacho/akitende.

Katika mazingira hayo mtoto atakuwa katika hali ya kuwa na roho ya kibinafsi, atakuwa ni mtu mwenye kujali hisia zake katika kila alitendalo kwa kuwa amezoea hivyo kuanzia utoto. Sasa unaweza kuona ni kwa jinsi gani kuna hatari kubwa, kuwa na jamii ambayo kila mtu anaweka hisia/maslahi yake mbele kabla ya wengine. Na ndiyo maana siku hizi imekuwa kawaida kuona vitoto vidogo vikiropoka au kufanya mambo ya ajabu na vinapokemewa vinatema shit kwa sababu ya aina ya makuzi ambayo vimekuwa vikipewa na wazazi wao. Na hivo hivo ndo baadaye vikija kuwa viwatu wazima vinakuwa vimtu vya hovyo hovyo tu.

Lakini kama upendo wa wazazi ukiwa na kikomo katika hatua hii ya mwanzo kabisa ya malezi, watoto wangejengwa katika misingi ya kuwa, si kila jambo ambalo wanalifanya, kulitamani ni sahihi. Wangekua katika misingi ya kuheshimu mawazo na ushauri kutoka kwa watu wengine.

MAISHA YA USASA, TISHIO JINGINE KWA USTAWI WA WATOTO

Nyakati zinasonga mbele, na maisha kwa kasi sana yanabadilikaa. Nasi kama najamii tunajitahidi kwa kasi ile ile kujaribu kuendana na mabadiliko hayo ili tusionekane tuko nyuma ya ulimwengu. Na ndiyo sababu si ajabu kukutana na post facebook za mashangazi huko vijijini wakiwa wamepiga picha na kuandika caption “usiku mwema wana fb”. Kila mtu anataka kwenda sawa na nyakati.

Hakuna anayekataa kuwa kwenda na wakati ni kuzuri, lakini kujaribu kufanya kila kitu kinachoonekana kinafanywa na watu wengi bila kupima madhara yake tatizo kubwa sama. Na ubaya zaidi ni kuwa katika mazingira kama haya hauwezi kujua kuwa ni tatizo hadi pale utakapopata madhara makubwa na huenda usijue yametoka wapi. Na katika moja ya kundi lililoathirika na litaendelea kuathirika na usasa ni kundi la wazazi na jamii kwa watoto wao.

Wazazi na jamii ya sasa tunawalea watoto kisasa mno. Tunawalea kiasi kwamba unashindwa kutambua huyu mtoto akikua atakuwa ni mtu wa aina gani. Tuchukulie mfano, mtoto wa kike wa miaka miwili hadi mitato unaanza kumpamba; unamsuka nywele, unampaka lipstic sijui wanja na makorokoro mengine mengi au mtoto wa kiume unamnyoa kiduku, wengine wanawavisha watoto wao hereni na wengine wanaenda mbali zaidi na kuwapaka nywele dawa. Kwa kuwa mtoto humwamini sana mtu ambaye yuko karibu naye basi pia huamini kuwa kila kitu anachokifanya mtu huyo ni sahihi. Sasa jiulize mtoto wa aina hii anafikisha miaka mitano na anatakiwa kwenda shule na akifika shule anatakiwa kuacha vile vitu ambavyo wazazi wake wamekuwa wakimfanyia tangu akiwa na miaka 2..ni lazima roho ya upinzani itaanza kujijenga pale taratibu.

Haiwezekani baba yake anayemlisha na kumvisha anampeleka saluni ananyolewa kiduku na anasifiwa na mama yake kuwa “mwanangu umependeza” halafu mwalimu tu ambaye wanaonana mchana aje amwambie kuwa kunyoa hivyo ni kinyume na taratibu halafu mtoto amuelewe kirahisi. Mtamlazimisha atafanya lakini ipo siku ambayo wazazi na jamii hamtakuwa na uwezo wa kum-control, unadhani nini kinatokea? Lakini chanzo ni kuwa wazazi walifanya aishi katika umri wa ujana ilhali yeye ni mtoto.

Binafsi, mtoto anatakiwa kuishi kama mtoto. Mtoto hatakiwi kuwa ni chombo cha kuonyeshea umaridadi wa familia, mtoto hatakiwi kuwa sehemu ya kujifunzia kuremba, mtoto hatakiwi kulelewa katika misigni inatoyofanya kundi la watu wanaojielewa kuhoji usahihi wa malezi anayopata, mtoto hatakiwi kuwa yai lilibebwa katikati ya fungu la sufu. Mtoto anatakiwa apewe upendo kwa kiasi anachostahili kulingana na hadhi yake ya ‘utoto’, mtoto anatakiwa arekebishwe mara tu anapokosea kulingana na mazingira ya kosa na uzito wa kosa lenyewe, kwa ufupi; mtoto na alelewe kama mtoto na si kama mtu mzima aliyedumaa kiumbo.

Haya ni maoni binafsi, naruhusu kukosolewa na kurekebishwa kwa nia njema.

Chelu, Stephen N.
-------------------

NAFASI ZA AJIRA 

JIUNGE NA AJIRA YAKO TELEGRAM GROUP HAPA

INTERNSHIP VACANCIES

GOVERNMENT VACANCIES

NGO'S VACANCIES 

GOODLUCK

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad