Korea Yaipatia Tanzania Mkopo Nafuu Wa Sh. Bilioni 684.6 Kutekeleza Miradi Mitano Muhimu

 AJIRA ZA UHAKIKA NJE NJE, BONYEZA HAPA

 


Na Josephine Majua na Ramadhani Kissimba – WFM - DODOMA

Serikali za Tanzania na Korea zimetiliana saini mkataba wa mkopo wenye masharti nafuu wa dola za Marekani milioni 300, sawa na shilingi za Tanzania bilioni 684.6, kupitia Mfuko wa Ushirikiano wa Kiuchumi wa nchi hiyo (EDCF), kwa ajili ya kugharamia utekelezaji wa miradi mitano ya maendeleo katika sekta za afya, maji, miundombinu na nishati.


Mkataba wa mkopo huo umesainiwa Jijini Dodoma na Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango, Bw. Doto James kwa upande wa Serikali na Balozi wa Korea hapa nchini Mhe. Cho Tae – Ick.


Ujenzi wa Vituo viwili vya kupooza Umeme

Bw. James alisema kuwa mradi huo utahusisha ujenzi wa Kituo cha kupooza umeme cha Kigoma cha msongo wa 400kv/132kv/33kv na upanuzi wa kituo cha kupooza umeme cha Nyakanazi cha msongo wa 400kv/220kv, utakao gharimu dola za Marekani milioni 45 sawa na shilingi bilioni 102.9


“Kukamilika kwa miradi hiyo kutaongeza umeme kupitia gridi ya Taifa na kupunguza changamoto ya upatikanaji wa umeme katika mikoa ya Kaskazani Magharibi ya Tanzania na itapunguza gharama ya uendeshaji na ukarabati wa mitambo ya kuzalisha umeme unaotumia mafuta ya dizeli” alisema Bw. James.


Kusaidia Bajeti Kuu ya Serikali, kukabiliana naathari za Covid-19

Bw. James alisema kuwa Serikali ya Jamhuri ya Korea, imetoa mkopo wa dola za Marekani milioni 40 sawa na sh. bilioni 91.4 kwa ajili kuboresha mfumo wa afya nchini kwa kuongeza uwezo wa kibajeti wa Serikali wa kukabiliana na madhara ya kibajeti yaliyotokana na ugonjwa wa korona.


Mradi wa Uboreshaji wa Huduma za Majitaka katika Jiji la Dodoma

Katibu Mkuu, Wizara ya Fedha na Mipango Bw. Doto James, alisema kuwa Korea imetoa dola za Marekani milioni 70 sawa na sh. bilioni 160 kwa ajili ya mradi huo unaolenga kuboresha mfumo wa majitaka jijini Dodoma.


“Mradi huu utahusisha ujenzi wa mtambo wa kutibu majitaka wenye uwezo wa kutibu mita za ujazo elfu 20 kwa siku, kuunganisha mabomba ya mfumo wa maji taka katika majengo ya ofisi, makazi, shule za msingi na Sekondari na utasaidia kukabiliana na ongezeko la watu baada ya Serikali kuhamishia makao yake Makuu Jijini Dodoma pamoja na kukabiliana na uchafuzi wa mazingira” alifafanua Bw. James.


Mradi wa Kuimarisha Miundimbinu ya Upimaji na Ramani wenye nchini.

Bw. James, alisema kuwa sehemu ya mkataba huo unahusisha dola za Marekani milioni 65 sawa na shilingi bilioni 148.6 kwa ajili ya mradi huo wenye lengo la kuimarisha na kuboresha miundombinu ya upimaji ardhi na ramani na unakusudia kujenga uwezo endelevu  wa Serikali  wa kuandaa ramani za msingi, kuongeza kasi na kupunguza gharama za upimaji ardhi.


Aliongeza kuwa mradi huo utahusisha ujenzi wa vituo 30 vya upimaji ardhi kwa njia ya kielektroniki katika miji mikuu ya mikoa na kuongeza alama 357 za upimaji ardhi nchini, kununua zana za kuandaa ramani, kujenga kanzidata ya taarifa za kijiografia na mifumo ya kulinda na kusambaza taarifa hizo kwa watumiaji wa mfumo huo.


Mradi wa Ujenzi wa Daraja jipya la Salender, Dar es Salaam

Bw. James, alisema kuwa Serikali ya Korea imetoa mkopo wa dola za Marekani milioni 32.6 sawa na shilingi bilioni 74.5 ikiwa ni nyongeza ya mkopo wa awali wa dola za Marekani bilioni 91.032 uliotolewa na nchi hiyo kwa ajili ya ujenzi wa daraja la Selander, Jijini Dar es Salaam baada ya fedha hizo kutotosha kukamilisha mradi huo.


Aidha aliongeza kuwa daraja hilo jipya linalojengwa linahusisha barabara unganishi zenye jumla ya kilomita 6.23, lengo lake likiwa ni kupunguza foleni ya magari katika Barabara ya Ali Hassan Mwinyi.


Aliishukuru Serikali ya Jamhuri ya Korea kwa kuendelea kushirikiana na Tanzania katika kusukuma kugurumu la maendeleo na kwamba hadi sasa miradi ya maendeleo inayotekelezwa ina thamani ya dola za Marekani milioni 258.03, sawa na sh. bilioni 589.89 katika sekta za afya, kilimo, madaraja, na sekta ya maji.


Kwa upande wake Balozi wa Korea nchini Tanzania, Mhe. Cho Tae- Ick, alisema kuwa nchi yake itaendelea kushirikiana na Tanzania katika kuchochea maendeleo ya wananchi wake na kwamba wawekezaji wengi kutoka nchini mwake wamevutiwa kuja kuwekeza nchini na kuitaka Tanzania kuchanganmkia fursa hiyo.


Aliahidi kuwa Korea itaendelea kushirikiana na Tanzania kwa njia mbalimbali ikiwemo kuipatia mikopo yenye riba ndogo sana ili iweze kutekeleza miradi yake muhimu kwa ajili ya ukuaji wa haraka wa uchumi wa nchi na kuboresha maisha ya wananchi kwa ujumla.


Naye Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maji Mhandisi Nadhifa Kemikimba, akishukuru kwa niaba ya wanufaika wanzake wa mkopo huo kutoka Wizara za Nishati, Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, na Wizara ya Ujenzi ambapo aliahidi kuwa watasimamia kikamilifu matumizi ya fedha hizo ili miradi iliyokusudiwa ikamilike kwa wakati na kwa ubora unaotakiwa.


Viongozi wengine walioshiriki hafla hiyo ni Mwakilishi mkazi wa Mfuko wa Ushirikiano wa Maendeleo ya Kiuchumi wa Korea Bi. Jo Younkyoung, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango, Bi. Amina Khamis Shaaban, Naibu Katibu Mkuu  Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Bw. Nicolaus Mkapa.


MWISHO.

-------------------

NAFASI ZA AJIRA 

JIUNGE NA AJIRA YAKO TELEGRAM GROUP HAPA

INTERNSHIP VACANCIES

GOVERNMENT VACANCIES

NGO'S VACANCIES 

GOODLUCK

Tags

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad