Prof. Manya atahadharisha Biashara ya madini nje ya masoko

 AJIRA ZA UHAKIKA NJE NJE, BONYEZA HAPA





Wanunuzi wa Madini ya Tanzania wametahadharishwa kutokununua Madini Nje ya Mfumo wa Masoko ili kuepuka kuuziwa madini bandia tofauti na wanapofanyabiashara ndani ya masoko kwani hakuna kificho.

Tahadhari hiyo imetolewa  Julai 25, 2021 na Naibu  Waziri wa Madini Prof. Shukrani Manya wakati akifungua Maonesho ya Pili ya Biashara na teknolojia kwa Mkoa wa Shinyanga kwa  niaba  ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Kassim Majaliwa .

Prof. Manya amesisitiza kuwa, mfumo wa biashara ya madini uliopo kwenye masoko yote 39 na Vituo vya Ununuzi wa Madini 50 yaliyoanzishwa mikoa yote nchini ni ya uwazi na hauruhusu madini bandia kuuzwa kwenye masoko hayo.

‘’ Mnaotaka kununua madini ya Tanzania msinunue nje ya mfumo wa masoko, nje ya masoko mnauziwa madini feki,’’ amesisitiza Prof. Manya.



Ameongeza kuwa kutokana na Tanzania kuonesha mageuzi makubwa kufuatia kuanzishwa kwa masoko ya madini, ndiyo nchi pekee duniani ambayo inaendesha biashara ya madini kwa uwazi kupitia masoko hayo jambo ambalo limeyafanya mataifa mengine duniani kutaka kujifunza.
 ‘’Wasiotaka kufuata taratibu ndiyo wanaokosoa mfumo wa masoko kwa kudhani Serikali imeyaanzisha ili kukusanya mapato. Wasiojua umuhimu wa masoko hayo waulizeni FEMATA na vyama vya wachimbaji kwenye mikoa watawaeleza,’’amesema Prof. Manya.

Ameongeza kuwa, Serikali itaendelea kuimarisha mifumo, sheria ili wananchi waendelee kunufaika na rasilimali madini na kuongeza kwamba, itaendelea kuimarisha masoko ya madini na kuyaongeza pale itakapohitajika.

Akizungumzia uzalishaji katika Mgodi Almasi Mwadui, Prof. Manya amesema uzalishaji katika mgodi huo uliathiriwa na janga la ugonjwa wa korona na hivyo kupelekea kusitishwa kwa uzalishaji lakini unatarajiwa kuanza tena uzalishaji wake mwezi Agosti, 2021.

Katika hatua nyingine, Prof. Manya amesema kuwa, Mkoa wa Shinyanga uko mbioni kuanzisha kiwanda cha kusafisha dhahabu kama ilivyo kwa mikoa ya Mwanza, Geita na Dodoma ili kuhamasisha shughuli za uongezaji thamani madini kufanyika nchini badala ya madini ghafi kusafirishwa katika nchi nyingine jambo ambalo litasaidia kuchochea ajira ikiwemo kuyapatia thamani halisi madini yanayozalishwa nchini.

Aidha, Prof. Manya ametumia fursa hiyo kuwaasa viongozi kuacha alama ya uongozi iliyotukuka kwa kufuata kanuni na misingi ya utawala bora ikiwemo kutoa kipaumbele katika usimamizi wa fedha za maendeleo kwa ajili ya manufaa ya wananchi na taifa kwa ujumla.

Akizungumzia kuhusu kuwaendeleza wachimbaji wadogo amesema kuwa serikali itaendelea kutenga maeneo kwa ajili ya wachimbaji   yenye taarifa za msingi za kijiolojia ili kuwawezesha wachimbe kwa tija.

Kuhusu ruzuku kwa wachimbaji wadogo Prof. Manya amesema awali, ruzuku iliyotolewa na Serikali kwa wachimbaji wadogo haikuleta tija iliyokusudiwa na kueleza kuwa, hivi sasa Serikali inaangalia namna bora ambayo itawezesha ruzuku hizo kuwa na tija. Ufafanuzi huo unafuatia ombi lililowasilishwa  na viongozi mbalimbali akiwemo Rais wa Chama Cha Wachimbaji wa Madini Tanzania (FEMATA) la kuwawezesha wachimbaji kupatiwa ruzuku.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Philemon Sengati amesema kuwa, katika Mwaka wa Fedha 2021/22 kuna uwezekano wa mkoa huo kukusanya mapato zaidi yanayotokana na rasilimali madini kutokana na kupatikana kwa maeneo mengine matatu kwa ajili ya shughuli za uchimbaji madini.

Ameyataja manufaa ya maonesho hayo kuwa ni pamoja na kubadilishana uzoefu, kuwakutanisha wazalishaji, wauzaji na walaji na kutoa mafunzo kwa wachimbaji wadogo , kuongeza mbinu  bora za kukuza sekta ya madini mkoani humo pamoja na  kutangaza fursa mbalimbali zilizopo katika mkoa huo.

Kwa upande wa wakuu wa Mikoa walioshiriki katika maonesho hayo wameleeza kuhusu kuunga juhudi za  mkoa huo,  kujifunza kuhusu namna mkoa unavyosimamia sekta ya madini na kubadilisha uzoefu.

Kwa upande wake, Rais FEMATA John Bina akizungumza katika ufunguzi huo, ameiomba Serikali ione namna ya kuwawezesha mafundi mchundo kupata mafunzo nje ya nchi ili kuwawezesha kujifunza kuhusu teknolojia bora ambazo zitawasaidia wachimbaji wadogo nchini kupata teknolojia rahisi kuendeleza shughuli zao.

Maonesho hayo yamehudhuriwa pia na wakuu wa mikoa kutoka mikoa jirani ikiwemo ya Mara, Tabora, Geita na Simiyu. Aidha, washiriki katika maonesho hayo ni kutoka sekta za umma, sekta binafsi, kampuni za madini, taasisi za kifedha, watoa huduma na wajasiliamali.

Maonesho ya Pili ya Biashara na teknolojia kwa Mkoa wa Shinyanga yanaongozwa na kaulimbiu ‘’Uwekezaji wa Madini na Viwanda Shinyanga kwa Uchumi Endelevu’. Maonesho hayo yaliyoanza tarehe 23 Julai, yanatarajiwa kuhitimishwa tarehe 1 Agosti, 2021.

 
-------------------

NAFASI ZA AJIRA 

JIUNGE NA AJIRA YAKO TELEGRAM GROUP HAPA

INTERNSHIP VACANCIES

GOVERNMENT VACANCIES

NGO'S VACANCIES 

GOODLUCK

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad