Mapya Yafichuka Rubi iliyo Mnadani Dubai

 AJIRA ZA UHAKIKA NJE NJE, BONYEZA HAPA



SERIKALI imetoa ufafanuzi juu ya jiwe la rubi linalosemekana kusafirishwa kwenda Dubai kutoka Tanzania kwa ajili ya kupigwa mnada na inafanya uchunguzi kujua mmliki halisi wa jiwe hilo na nchi lilipotoka.

Hayo yalielezwa na Waziri wa Madini, Doto Biteko alipokuwa akizungumza jijini Dodoma katika semina ya madini kwa wabunge wanawake.

Biteko aliwataka Watanzania wawe watulivu wakati serikali inaendelea kufanya uchunguzi kujua kama kweli jiwe hilo pamoja na mengine 25 yaliyogundulika baadaye yanatoka Tanzania kwa kuwa serikali haiwezi kutoa majibu ya haraka bila kujua lengo la taarifa hiyo iliyotangazwa kupitia kituo cha televisheni cha News24 Akifafanua jambo hilo.

Biteko alisema baada ya kuona taarifa hiyo kwenye mitandao walichukua hatua ya kuhakiki katika mfumo wa usafirishaji madini lakini hakukuwa na taarifa ya kusafirishwa jiwe hilo kwenda Dubai hivyo wakaamua kuwasiliana na kampuni ya SGA Dubai inayohusika na jiwe hilo wakawaeleza kuwa jiwe hilo walilipata kutoka Marekani.


“Kwanza kwepa (kukwepa na ujanja) zikawa nyingi kama kawaida tukawaambia kama serikali tunataka kutoa kauli juu ya hili jiwe ndiyo wakatupokea wakatuambia hili jiwe halikutoka Tanzania limetoka Marekani na Marekani nani kaliuza wakatuambia muuzaji anaitwa fulani, sitaki kumtaja kwa sababu bado tuko kwenye vikao tunaendelea,” alisema Biteko.

Alisema baada ya majibu hayo walituma maofisa ubalozi wakaenda SGA wakafanya kikao ambacho kilitoa taarifa kuwa ni kweli jiwe hilo lilitoka Tanzania hivyo walifanya mawasiliano na mhusika huyo wa Marekani ambaye walimtaka awasilishe nyaraka za utambulisho wa madini pamoja na kibali cha kusafirisha madini hayo lakini mhusika alipeleka nyaraka za Marekani badala ya Tanzania.

“Wakatuletea nyaraka kutoka GIA ya Marekani lakini hata hiyo certificate yenyewe nayo ina matatizo jiwe limetangazwa lina kilo 2.8 wao wanaonesha kilo 3.4. Tukawaambia tuleteeni certificate ya Tanzania na siyo ya Marekani wakasema hiyo ya Tanzania hatuna,” alisema. Alisema katika vikao walivyoendelea kufanya na pande zote mbili Dubai na Marekani waligundua kuwa kulikuwa na mawe mengine 25 yenye uzito tofauti ambayo hayakutolewa ufafanuzi mzuri zaidi ya kusema kuwa waliyapata Tanzania miaka 11 iliyopita.


Sintofahamu hiyo ndiyo iliyosababisha Biteko kuwataka Watanzania kuwa watulivu mpaka watakapokamilisha uchunguzi na kujua nia ya watu hao kutumia jina la Tanzania katika biashara hiyo kwani kuna uwezekano mawe hayo kuwa hayakutoka Tanzania kama inavyodaiwa.

Alifafanua kuwa utaratibu wa kuuza madini katika soko la dunia unafuata vigezo maalumu yakiwemo madini hayo kuchimbwa katika nchi ambayo haina machafuko ya aina yoyote na pia yachimbwe kwa kufuata maadili bila kuvunja haki za binadamu hivyo upo uwezekano wa nchi nyingine zisizo na sifa ya kuingiza madini yao katika soko la dunia wakatumia jina la Tanzania.

“Niwaombe ndugu Watanzania tutakapokamilisha tutatoa maelezo yenye pande zote mbili tutatoa nyaraka, tutatoa vithibitisho, kwa sasa kusema la nani siyo la nani itakuja mwishoni kuonesha hili jiwe ni la nani na mambo gani yako nyuma yake ili Tanzania tubaki kuwa salama.

“Nitakuwa Waziri wa ajabu sana nitakayekwenda kuchukua pendekezo walilotoa, nitawaeleza, kwa sababu kama watu wanasema bwana nyie mkubali tutumie jina lenu tutawapa dola milioni 20, unatupa dola milioni ishirini kwa kipi? Tunataka tujue kwanza hilo jiwe limetoka wapi hilo ndiyo jambo la msingi, mambo mengine yatakuja,” alisema.

Kwa nyakati tofauti wabunge hao walitaka ukweli wa mambo ujulikane ni kwa nini jiwe hilo linafichwa na kuhoji ni namna gani lilitoroshwa kutoka Tanzania. Madai kuhusu jiwe hilo la rubi lenye uzito wa kilo 2.8 linalotajwa kuwa litaingia sokoni kuuzwa siku 30 baada ya mfungo wa mwezi mtukufu wa Ramadhan, mara ya kwanza yaliibuliwa bungeni Aprili 21, mwaka huu na Mbunge wa Mkinga, Dustan Kitandula.

Mbunge huyo aliomba kufahamu kuhusu uvumi wa taarifa za mitandao wa jiwe hilo kubwa lenye thamani ya dola za Marekani milioni 120 sawa na Sh bilioni 240 na akahoji iwapo kuna ukweli wowote kuhusu jiwe hilo na ni namna gani Watanzania walinufaika na kodi yake.

Akijibu swali hilo, Naibu Waziri wa Madini, Dk Stephen Kiruswa alisema serikali ilipata taarifa za uwepo wa jiwe hilo tangu Aprili 13, 2022 na kwamba ilifanya mawasiliano na Ubalozi wake Dubai na ndipo katika kufuatilia, wakabaini kuwa mmiliki wake anatoka nchini Marekani katika mji wa California.

Habari Leo


-------------------

NAFASI ZA AJIRA 

JIUNGE NA AJIRA YAKO TELEGRAM GROUP HAPA

INTERNSHIP VACANCIES

GOVERNMENT VACANCIES

NGO'S VACANCIES 

GOODLUCK

Tags

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad