Lowassa,Mbowe na Sumaye Walilia Demokrasia Mbele ya Jeneza la Ndesamburo..!!!

 AJIRA ZA UHAKIKA NJE NJE, BONYEZA HAPA


Mawaziri wakuu wastaafu, Edward Lowassa na Frederick Sumaye jana walitema cheche katika shughuli ya kuaga mwili wa mbunge wa zamani wa Moshi Mjini (Chadema), Philemon Ndesamburo.

Mawaziri hao katika salamu zao za rambirambi walielezea masikitiko yao juu ya chuki kubwa inayopandikizwa nchini na pia jitihada zinazoendelea za kukandamiza demokrasia.

Hata hivyo, hakuna kiongozi yeyote wa Serikali aliyehudhuria shughuli hiyo hali ambayo ilionekana kuibua minong’ono kwa baadhi ya waombolezaji.

Mwenyekiti mwenza wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), James Mbatia alienda mbali zaidi na kusema hakukuwa na uwakilishi wa CCM unaofanana na sifa ya Ndesamburo aliyependa amani.

Katika hafla hiyo ya kumuaga kitaifa iliyofanyika uwanja wa Majengo, wabunge wa CCM waliwakilishwa na mbunge wa viti maalumu, Ester Mmasi aliyedai kuiwakilisha pia CCM.

Hotuba ya Mbowe

Hotuba ambayo iligusa hisia za waombolezaji wengi ni ya mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe aliyesema hatua ya viongozi wa Serikali na CCM kutohudhuria si tukio la bahati mbaya.

“Leo tumejenga Taifa lenye hofu. Watu wamekuwa waoga kwa sababu viongozi wameingiza hofu katika Taifa letu. Watu wenye hatia wana hofu. Kukosekana kwa uwakilishi wa Serikali mahali hapa si ajabu,” alisema Mbowe na kuongeza:

“Ni hofu ya hatia. Kwa heshima sana dada yangu Mmasi (Ester) pole. Asante sana kwa kufika. Umekuja hapa na kujaribu sana unamwakilisha sijui Serikali, sijui Rais. Hakuna.”

Mbowe alisema ameona vituko vingi katika msiba wa Ndesamburo kiasi kwamba anajiuliza inakuwaje wakati alikuwa mtu mwema na walitamani hata kumsindikiza kwa bendi ya polisi. “Tukaenda Chuo cha Polisi kuomba bendi ambacho mzee (Ndesamburo) anawasaidia mambo mbalimbali. Brass band hii inakodishwa kwa Sh300,000, tulikuwa tayari kulipa gharama hiyo,” alisema Mbowe na kuongeza:

“Mkuu wa chuo anaogopa kutoa Brass band ananiambia mwenyekiti Mbowe ongea na IGP (mkuu wa Jeshi la Polisi). Yaani Mbowe nimpigie IGP simu kumuomba Brass band (bendi ya polisi), mimi?”

“Leo polisi wanaogopa kufanya kazi kwa sababu hawajui bwana mkubwa atafurahi ama atakasirika. Ni mambo ambayo si ya Kitanzania. Tukahitaji kiwanja cha kumuaga baba nacho tukanyimwa.”

“Si kwamba kiwanja hiki cha Majengo hakifai. Ila kwa historia ya Moshi, uwanja wa Mashujaa kama unavyoitwa unastahili kuwa uwanja wa kuagwa mzee wetu Ndesamburo. Polisi wakaweka mizengwe.”

Mbowe alisema alifanya juhudi kubwa ikiwamo kuwasiliana na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa ambaye alimueleza kuwa anashughulikia, lakini hata hivyo ilikuwa ahadi hewa.

“Tulisema baba yetu ni kiongozi wa watu na sio wote wataweza kuja uwanjani. Tukaona ni haki tumpitishe (Ndesamburo) katikati ya mji lakini usiku tukaletewa barua ya zuio la polisi,” alisema.

“Kuna kiburi kinajengwa sana mikoa ya Kilimanjaro na Arusha. Naomba nimpelekee salamu mheshimiwa Rais, Watanzania wote sisi ni ndugu,” alisisitiza Mbowe ambaye ni mbunge wa Hai.

“Mwalimu (Nyerere) alitujenga tukawa tunapendana, lakini utawala huu wa awamu ya tano unafanya matendo yanayoonyesha ubaguzi na tunaona uonevu usiohimilika kwa mikoa ya Kilimanjaro na Arusha”.

Mbowe alisema ingawa watu wengi wanaogopa kuyasema hayo, yeye atayasema ili Rais, Waziri Mkuu na Serikali nzima ielewe kuwa Kilimanjaro na Arusha ni sehemu ya Tanzania.

“Watu wengi wanaogopa kusema. Siku hizi hata unaogopa kusema wewe ni Mushi. Uongo? Siku hizi watu wanaogopa kujiita Masawe, kujiita Tarimo kwa sababu huna uhakika watawala watafanya nini.”

“Hatuhitaji kujenga Taifa lenye ubaguzi, tunahitaji kumheshimu na kumthamini kila Mtanzania bila kujali dini yake, kabila lake wala jinsia. Tumuenzi Ndesamburo kwa kupendana,” alisema Mbowe.

Mbowe alisema Ndesamburo katika uhai wake alifanya mambo mengi na alikuwa mfadhili mkubwa si kwa Chadema pekee, bali watu wengi na makundi mbalimbali.

“Wakati polisi wanakuja kutufukuza katika uwanja wa Mashujaa na mabomu. Tukawaambia gari mnaloendesha tairi amenunua Ndesamburo. Na ni ukweli, sio nasema maneno ya uongo.”

“Huyu baba amejenga Mawenzi (hospitali) nani asiyejua. Amesaidia taasisi mbalimbali za dini, Wakristo na Waislamu. Amesaidia mashule sio tu kwa mkoa wa Kilimanjaro hata mikoa mingine.”

Mbowe alisema pamoja na kujitoa kwake huko, wako watu wanashindwa kuona thamani yake kwa sababu ya itikadi za kisiasa na kusisitiza kuwa siasa ni mambo ya mpito, lakini jamii itabaki.

“Leo sisi tunazika huku, bungeni wanamsimamisha Halima Mdee na Ester Bulaya. Hatuwezi kujenga Bunge la vibogoyo. Hatuwezi kujenga Bunge la wabunge waoga,” alisisitiza kiongozi huyo wa upinzani.

“Hii nchi imefika hapa kwa sababu kuna watu waoga na wenye hofu. Ugomvi wa Ester Bulaya na Halima Mdee ulianza wakati wa bajeti ya Nishati na Madini.”

“Katika mjadala ule mheshimiwa Mnyika (John) kaamriwa kutoka nje na spika kwa uonevu ulio dhahiri. Wabunge wale akina mama wakasimama wakasema huyu mtu hatendewi haki. Wabunge msifungwe midomo na mkienda bungeni wabunge wote msimame imara na Watanzania bila kujali vyama vya siasa tuitake nchi hii ijifunze kuhoji viongozi wanapofanya makosa.”

Mbowe alitumia hadhara hiyo kutuma salamu kwa wale aliosema wanafikiri kuondoka kwa Ndesamburo ni kuterereka kwa Chadema akisema haitatokea na wataendelea kuijenga vyema Moshi.

Sumaye, Lowassa na Mbatia

Sumaye ambaye ndiye aliyeongea kwa kirefu alisema Afrika itaendelea kama Serikali zilizo madarakani zitaenzi demokrasia na kuachia madaraka kwa amani badala ya kung’ang’ania.

“Kuna juhudi kubwa sana zinaendelea za watu kujidanganya kuwa wanaweza kukandamiza demokrasia. Hapa demokrasia ilipofikia huwezi tena kuikandamiza,” alisema Sumaye na kuongeza:

“Mpira una bladder (puto) ndani. Ukiikandamiza sana itapasuka na ikipasuka itakuwa na madhara makubwa. Tuache Watanzania wafurahie demokrasia katika nchi yao. Hili ni muhimu.”

“Tuache kupandikiza chuki. Mikutano ya siasa inazuiwa, njia za kupitisha maiti (ya Ndesamburo) zinazuiwa. Hatuwezi kuwaonea wananchi hawa kwa muda mrefu.”

Lowassa aliunga mkono maneno yaliyosemwa na Sumaye kuhusu jitihada kubwa zinazoendelea za kudidimiza demokrasia na kupandikiza chuki katika jamii.

“Jitihada za kudidimiza demokrasia inaendelea sana. Hawa waliozuia tusiagie Mashujaa tuwasamehe. Hupimi watu kwa uwanja, bali kwa roho zao,” alisema Lowassa aliyegombea urais mwaka 2015 kupitia Ukawa.

Awali, katika hotuba yake Mbatia alilaani tabia iliyoanza kujengeka ya kuwafarakanisha Watanzania na kumtaka Rais Magufuli ajue kuwa Tanzania ni ya Watanzania wote.

Mbatia ambaye pia ni mbunge wa Vunjo (NCCR-Mageuzi) alitoa mfano wa tukio la Aprili 30, wakati Rais alipofanya ziara mkoani Kilimanjaro ambapo meya na mbunge walitimuliwa Ikulu.

“Mbunge wa Moshi Mjini (Jaffar Michael) na meya wa Moshi (Raymond Mboya) wakaondolewa Ikulu na Rais akakaa kimya tu. Tanzania ni mali ya Watanzania na sio ya John Pombe Magufuli,” alisema.

“Tangu tumeanzisha mageuzi haya labda John Magufuli alikuwa shule, lakini hatuwezi kukubali Taifa letu likasambaratika kwa maslahi ya watu wachache,” aliongeza kusema na kusisitiza:

“Rais akija Moshi, mwenyeji wako ni meya na mbunge, watu wako wa usalama hawawezi kuwaondoa.

“Niwaombe CCM, Tanzania ni mali ya Watanzania wote, nitaongea nao. Kitendo walichofanya leo sio utamaduni wa Watanzania. Sioni uwakilishi wa CCM unaofanana na Ndesamburo.”

Makamu Mwenyekiti wa CUF, Severina Mwijage alisema wale wote waliozuia Ndesamburo asiagwe katika Uwanja wa Mashujaa Mungu atawalipa kwa kile walichokifanya.

“Huwezi kuwachonganisha wananchi namna hii. Chadema mna salamu inasema peoples power. Tungeamua kutumia nguvu ya umma msingeweza (polisi) kufanya lolote,” alisema.

Kiongozi wa ACT Wazalendo, Zitto Kabwe alipendekeza halmashauri ya manispaa ya Moshi inayoongozwa na Chadema kutafuta mtaa bora ndani ya mji na upewe jina la Ndesamburo.

Zitto alisema hiyo itakuwa ni njia bora ya kuenzi mchango mkubwa wa Ndesamburo katika jimbo hilo ili mtu yeyote akifika Moshi ajue jabali la siasa alikuwa anaishi mjini humo.

Katika shughuli hiyo ya kuaga mwili wa Ndesamburo, waziri wa zamani wa fedha na mbunge wa zamani wa Rombo (CCM), Basil Mramba alikuwa kivutio alipoingia uwanjani hapo.
----

Utamu wa audio book ya SIRI YA PADRE NA MKE WANGU hauna mfano, sikiliza Sehemu ya 1 bure, Sehemu ya 2 Tsh 2000 tu

Nusu ya mapato ni kwa ajili ya wagonjwa wasiojiweza, Lipia uburudike huku ukitoa sadaka Safi,ni www.makapedia.com au bofya kitabu hapo chini:



 

-------------------

NAFASI ZA AJIRA 

JIUNGE NA AJIRA YAKO TELEGRAM GROUP HAPA

INTERNSHIP VACANCIES

GOVERNMENT VACANCIES

NGO'S VACANCIES 

GOODLUCK

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad