Makamo wa rais wa Kenya, William Ruto, anasema kuwa askari wa usalama wa Kenya wamewaandama wapiganaji wa al-Shabaab hadi kwenye kambi yao nchini Somalia, baada ya shambulio dhidi ya basi kaskazini-mashariki mwa Kenya hapo jana ambapo raia 28 waliuliwa. Bwana Ruto alisema wapiganaji zaidi ya 100 waliuliwa katika operesheni mbili tofauti. Alisema kambi ya al-Shabaab iliangamizwa. Habari hizo hazikuthibitishwa na upande wa pili. Gavana wa Mandera - ambako shambulio la jana lilitokea - amelaumu vikosi vya usalama kwa kushindwa kuwalinda raia. Alisema polisi kawaida wanashindwa kufanya uchunguzi kamili baada ya mashambulio.