Mchechu adai fidia bil. 3/- madai kuchafuliwa "Sikuwahi Kufukuzwa Kazi na Magufuli"

 AJIRA ZA UHAKIKA NJE NJE, BONYEZA HAPA



MKURUGENZI Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), Nehemiah Mchechu, amefungua kesi katika Mahakama Kuu ya Tanzania, akiombwa kulipwa fidia ya Sh. bilioni 3 na gazeti la The Citizen kwa madai ya kuandika habari zilizomchafua na kumshushia hadhi kitaifa na kimataifa.


Kesi hiyo ilianza kusikilizwa Ijumaa iliyopita jijini Dar es Salaam mbele ya Jaji Leila Mgonya wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam. Katika kesi hiyo, Mchechu anawakilishwa na mawakili wa kujitegemea Aliko Mwamanenge ma Vitalis Peter.

Mchechu anadai kuwa gazeti hilo katika toleo lake la Machi 23, 2018, lilichapisha habari yenye kichwa kinachosomeka ‘Why JPM dissolved NHC Board, sacked Mchechu’, kwa tafsiri isiyo rasmi ‘Kwa nini JPM (John Magufuli- aliyekuwa Rais) alivunja Bodi ya NHC, kumfukuza Mchechu’.

“Machi 23, 2018 ilikuwa siku ya kiza kwangu. Ni siku ambayo niliandikwa na gazeti la the Citizen ukurasa wa mbele habari ambayo ililenga kunichafua, kunishushia hadhi, kunikosanisha na jamii kubwa ya Watanzania na kuonekana kuwa ni mtu nisiyefaa kabisa kuwa kiongozi au sehemu ya jamii njema ya Watanzania. Mtu nisiye na maadili, nisiyeaminika na kimsingi nisiyestahili hata kuongoza popote,” alidai Mchechu alipoongozwa na Wakili Peter katika kutoa ushahidi wake.

Mchechu ambaye alirejeshwa katika nafasi hiyo miezi kadhaa iliyopita na Rais Samia Suluhu Hassan baada ya kuondoka mwaka 2018, alidai kwamba habari hiyo ina upotoshaji mkubwa kimantiki na kimaudhui kwa kuwa hajawahi kufukuzwa kazi kama ilivyodaiwa.


“Gazeti hili liliandika habari likijua sijafukuzwa, kwa kuwa sijafukuzwa kazi na wala Mheshimiwa Rais hakuwa na hakuwahi kunifukuza kazi. Kwa hiyo hii ilikuwa habari ya uongo na yenye nia ovu ya kunichafua na kunishushia hadhi yangu katika familia yangu, taifa na duniani kwa ujumla,” alidai.

CHANZO CHA MADAI

Katika habari hiyo iliyobeba habari kubwa ukurasa wa mbele ya kuwekwa ukurasa wa nne, ilidaiwa kuwa Mchechu alikuwa akichunguzwa na Bodi ya NHC na kuhojiwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) juu ya mgongano wa kimaslahi juu ya utafutaji na upatikanaji wa ekari 500 za mradi wa NHC wa Safari City jijini Arusha.

Ilidaiwa kuwa ardhi hiyo, awali iliripotiwa kununuliwa na kampuni inayomilikiwa na Mchechu ambayo iliinunua kutoka kwa raia wa kigeni na uchunguzi ulionyesha kuwa aliiuzia NHC kwa bei ya juu.

Pia kwa mujibu wa habari hiyo, Mchechu alidaiwa kumtumia mkandarasi wa NHC kutengeneza barabara kwenda kwenye eneo lake lililo karibu na eneo la mradi wa Safari City huku gharama zikiwa zinabebwa na shirika.

Sambamba na hayo, taarifa hiyo ilidai kuwa kampuni ya PHILS International ya Dubai ilipewa kazi katika mradi wa Kawe kwa uamuzi wa Mchechu bila kumhusisha Mkuu wa Kitengo cha Ununuzi cha NHC, Hamis Mpinda.

Aidha, habari hiyo ilidai kuwa uchunguzi ulikuwa unafanywa kuhusu madai ya kampuni ambayo mke wa Mchechu ni mkurugenzi kupewa mkataba wa kutoa bima kwa ajili ya nyumba za shirika mkoani Mtwara jambo ambalo ni kinyume cha kanuni za utumishi wa umma juu ya mgongano wa kimaslahi.

Kadhalika, kwa mujibu wa habari hiyo, vyanzo vya habari vilibainisha kwamba kamati iliyoundwa kuchunguza matumizi mabaya ya ofisi ndani ya NHC ulionyesha ukiukwaji mkubwa na matumizi mabaya ya kutisha ya fedha za umma uliofanywa na Mchechu.


USHAHIDI WA MCHECHU

Katika ushahidi wake mahakamani juu ya habari hiyo, Mchechu alidai kwamba haina hata chembe ya ukweli isipokuwa ililenga kumchafua na kumharibia heshima yake aliyoijenga katika jamii kwa muda mrefu.

Alidai kuwa kulingana na madai ya habari hiyo, NHC haijawahi kununua ekari 500 jijini Arusha kwa ajili ya mradi wa Safari City bali ekari halisi ni 583 na kwamba hajawahi kuchunguzwa kutokana na bodi ya shirika au taasisi yoyote ya uchunguzi ikiwamo TAKUKURU kuhusu mradi huo na kwamba hana ardhi karibu na mradi huo kama ilivyodaiwa.

Mchechu alidai kwamba ardhi anayodaiwa kuiuzia NHC si kweli kwa kuwa hajawahi kumiliki ardhi katika mkoa wa Arusha katika maisha yake wala hana kampuni iliyowahi kufanya hivyo. Pia alidai hajawahi kuiuzia NHC ardhi popote Tanzania.

Pia alidai kwamba hawajahi kuingilia masuala ya ununuzi akiwa mtendaji mkuu wa shirika na hajawahhi kupoka mamlaka hayo. Kuhusu madai ya kampuni ya mke wake, alidai kwamba halijawahi kufanyika jambo kama hilo na kwamba NHC haikati bima kwa ajili ya mali zake zikiwamo nyumba.

Kuhusu uchunguzi wa matumizi mabaya ya ofisi na matumizi mabaya ya fedha za umma, bosi huyo wa NHC alidai kuwa hakuna kitu kama hicho na hakujawahi kuwapo taarifa ya uchunguzi iliyomtia hatiani kwa matumizi mabaya ya fedha za umma na ukosefu wa maadili.

ATHARI

Kutokana na habari hiyo, Mchechu alisema licha ya kumshushia hadhi, alikosa kuaminika, hivyo kupoteza nafasi nyingi za kibiashara alizokuwa anafanya pamoja na kuondokewa na wabia katika kampuni ambazo ana uhusiano nazo kibiashara.

“Taarifa hii ilinisababishia mfadhaiko mkubwa wa akili, msongo wa mawazo hofu na kudhuru afya yangu. Pia ilinipotezea nafasi ya maendeleo yangu kikazi na kunipotezea mapato ya ajira yangu na ushiriki wangu katika bodi mbalimbali ndani na nje ya nchi,” alidai huku akiongeza kuwa alilazimika kujiuzulu baadhi ya nyadhifa.

Mchechu pia alidai mahakamani kwamba wakati habari hiyo inaandikwa alikuwa katika mchakato wa kupata nafasi ya ofisa mtendaji mkuu wa taasisi ya kimataifa ya kifedha ya Shelter Afrique, hivyo kusababisha kukosa licha ya kwamba alikuwa akiongoza katika mchakato huo.

Pia kutokana na nafasi yake ya uongozi katika kanisa, akiwa Mwenyekiti wa Halmashauri ya Fedha ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya Mashariki na Pwani, alikosa kuaminika na kuwapo hofu ya usalama wa sadaka za waumini.


“Kwa kweli habari hii imenifanya nionekane mlafi, tapeli, mlanguzi, mtu anayetumia vibaya nafasi yake. Pamoja na mambo mengine, naiomba mahakama nisafishwe na chombo hiki na nilipwe fidia kutokana na athari na hasara nilizopata,” alidai.


----

Love Story ya NJIA PANDA,Ni Kali mnoo Jamani.

Kusikiliza au kusoma mwendelezo wake Tembelea www.makapedia.com kisha bofya palipoandikwa NJIA PANDA kila siku saa moja kamili jioni BURE au bofya HAPA

Pia Bofya HAPA kujiunga na what's app channel yetu,tukukumbushe kila siku.


-------------------

NAFASI ZA AJIRA 

JIUNGE NA AJIRA YAKO TELEGRAM GROUP HAPA

INTERNSHIP VACANCIES

GOVERNMENT VACANCIES

NGO'S VACANCIES 

GOODLUCK

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.

Top Post Ad