KWA MWENENDO HUU, TAIFA STARS ITAFUNGWA KILA SIKU MPAKA MABADILIKO YAFANYIKE…..!

 AJIRA ZA UHAKIKA NJE NJE, BONYEZA HAPA


KIKOSI cha timu ya soka ya taifa ya Tanzania, maarufu kama Taifa Stars juzi kilipoteza mechi yake ya kuwania kufuzu Kombe la Mataifa ya Afrika kwa Wachezaji wa Ndani (CHAN) kwa kufungwa bao 1-0 dhidi ya Uganda, The Cranes kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Kabla ya mchezo huo, matarajio ya wengi yalikuwa ni Taifa Stars kuibuka na ushindi kutokana na muonekano wa mechi yenyewe na rekodi ya Taifa Stars kwa siku za hivi karibuni. Sasa matumaini ya Taifa Stars kucheza CHAN ni madogo mno kulinganisha na hali ilivyokuwa hapo awali.
Hii ina maana, Taifa Stars inatakiwa kupata ushindi usiopunguwa bao 1-0 kwenye mechi ya marudiano itakayochezwa wiki mbili zijazo kwenye Uwanja wa Namboole huko Uganda.
Mengi yalitokea katika mchezo wa jana, ambao uliwatoa vichwa chini Watanzania wengi waliodhani timu yao ingeweza kufanya vizuri baada ya hivi karibuni kuwa na matokeo ya kuridhisha.
  
TAIFA STARS ILIWAKOSA WAWILI, UGANDA ILIWAKOSA KUMI….LAKINI BADO MAMBO YAKAWA MAGUMU KWAO

Taifa Stars iliingia uwanjani ikiwa imewakosa wachezaji wake wawili tu wa kikosi cha kwanza kutokana na kanuni kuwabana, nao ni Mbwana Samatta na Thomas Ulimwengu wanaochezea TP Mazembe ya DR Congo.
Samatta na Ulimwengu hawakuweza kucheza mechi hiyo kutokana na ukweli kwamba, hiyo ni michuano maalum kwa wachezaji wa ligi za ndani ya nchi pekee.
Shirikisho la Soka Afrika, CAF lilianzisha michuano hii ili kutoa fursa kwa wachezaji wanaoshiriki ligi za ndani za nchi zao nao kuonekana na kutoa michango yao kwa timu zao za taifa ambazo mara nyingi zilikuwa zikisheheni wachezaji wanaocheza nje ya Afrika.
Wachezaji wanaocheza ligi za ndani katika nchi kama Nigeria, Ivory Coast na Senegal, huwa hawapati nafasi ya kucheza michuano ya aina yoyote katika vikosi vya nchi hizo ambavyo husheheni idadi kubwa ya wachezaji wanaocheza soka la kulipwa nje ya Afrika hasa Ulaya.
Kwa kutambua hilo, CAF ikaamua kuanzisha michuano hii ya CHAN ambayo Tanzania imeshiriki mara moja na Uganda pia imeshiriki mara moja. Kwa kutaka michuano hii ichezwe na timu kutoka pande zote za Afrika, CAF ikawa inahakikisha kila pembe ya Afrika inashiriki michuano hii, ndiyo maana leo Tanzania na Uganda zinawania nafasi ya kufuzu kucheza fainali hizo.
Wakati Taifa Stars ikiwakosa wachezaji wawili tu, Uganda iliwakosa wachezaji kumi (10) ambao mara nyingi huwamo katika kikosi cha kwanza cha timu hiyo. Hii ina maanisha Uganda ilikuwa na wachezaji wawili tu wa kikosi cha kwanza kinachojumuhisha hata nyota wanaocheza nje ya Uganda.
Wachezaji wa Uganda waliocheza mechi ya jana ambao mara nyingi huchezea timu ya taifa ni Hamza Muwonge na Hassan Waswa ambaye jana alikuwa nahodha. Wengine wote waliocheza jana, huwa hawana nafasi katika kikosi cha Uganda. Kazi ipo.
    
TANZANIA LIGI DUNI, UGANDA LIGI BORA….

Kwa matokeo ya mechi ya jana, imedhihirika wazi kwamba Ligi Kuu ya Tanzania Bara, haina ubora kulingana na ile ya Uganda. Wachezaji wengi wa Taifa Stars hawakuweza kucheza vizuri mbele ya wenzao wa Uganda walioweza kutawala na kucheza kwa malengo katika eneo la kiungo kwa muda mwingi.
Kabla ya mchezo ilionekana wachezaji wa Tanzania wangeweza kuwapiku wa Uganda lakini muda mfupi baada ya mchezo kuanza, ubora wa wachezaji wa Uganda ulikuwa ukitawala kila mara. Viungo kama Salum Aboubakar ‘Sure Boy’, Frank Domayo, Amri Kiemba, Mrisho Ngassa na Mwinyi Kazimoto hawakuweza kuwa imara na kuisaidia timu.
Bado wachezaji hao wanacheza na majukwaa huku wakipoteza malengo ya timu mara kwa mara hasa kwa kukariri mfumo wa kucheza pasi za nyuma wakati timu ikipanda, na hata uanzishwaji wa mipira mara nyingi umekuwa ule ule, kwamba mpira anaanziwa Aggrey Morris au Kelvin Yondani halafu utaenda kwa Erasto Nyoni, naye ataupeleka kwa Sure Boy halafu Sure Boy anaupeleka kwa Shomari Kapombe au unarudi tena kwa Morris ambaye ataupiga juu katikati halafu John Bocco atashindana nguvu na mabeki wa Uganda kisha anaupoteza halafu kazi ya kukaba inaanza.
Kwa mchezo wa jana wa Taifa Stars, hakika kila siku tutalia kama hatutakubali kufuata yafuatayo;
KUREKEBISHA MFUMO WA SOKA TANZANIA…
Timu zote tunazocheza nazo kisha zikatufunga, ukizitazama utagundua zina mfumo wa kuopoa vipaji vya wachezaji wake, hasa kuanzia ngazi ya shule za msingi, sekondari hata katika vyuo vikuu.

Mtazame mfungaji wa bao pekee la Uganda, Dennis Guma huyu anatokea timu ya Victoria University ambayo pia inashiriki Ligi Kuu ya Uganda. Timu hii ina timu kibao za watoto wadogo ambao wanapitia katika mfumo mzuri wa soka na hata kupata elimu ya dunia kwa pamoja.
Leo hii wachezaji wengi kutoka Kenya au Uganda mpaka wanapofikia hatua ya kucheza Ligi Kuu wengi wao ni agharabu kuwakuta na elimu chini ya kidato cha nne au kidato cha sita kutokana na mfumo wao wa elimu dunia na ile ya michezo hasa soka. Siwakosoi kwa kutokuwa na elimu, lakini utawasikia wameshindwa kuendelea na elimu ya sekondari kutkana na matatizo ya kifamilia.
Academy nyingi za nchi hizo, zinawapa fursa wachezaji kupata elimu zote hizo (soka na elimu ya darasani) kwa pamoja na ndiyo msingi wa mafanikio yao leo hii. Hao wanakua kiakili huku wakijua namna ya kupokea mafundisho.
Hapa kwetu leo hii kitazame kikosi cha Taifa Stars, kisha omba rekodi za walipotokea wachezaji wake halafu uliza kuhusu elimu zao, utashangaa, lakini ndiyo aina ya wachezaji tulionao. Tufanyeje? Hakuna jinsi.
Wachezaji wengi wa Taifa Stars hawajulikani wanapotokea, unashtukia mtu anacheza Simba, Yanga au Azam au hata timu nyingine ya ligi kuu bila hata ya kucheza mechi moja ya ligi daraja la tatu au ile ligi ya taifa. Sasa huyu atawezaje kupambana na mtu aliyepitia mfumo sahihi wa soka? Huu ni utani.
Siyo siri, Taifa Stars inaundwa na wachezaji wengi wa Simba, Yanga na Azam, lakini ni Azam pekee yenye mfumo mzuri wa usajili wa wachezaji kwa kuwa na academy yake inayozalisha wachezaji kila siku. Hizo Simba na Yanga bado zina mfumo wa kuita lundo la wachezaji katika mazoezi yao na kutazama uwezo wao kisha kuwasajili.
Sipo hapa kuisifia timu fulani au kuiponda timu nyingine, natoa machungu yangu ya rohoni kutokana kuumizwa na kipigo cha jana cha Taifa Stars dhidi ya Uganda iliyoonekana kuwa dhaifu pengine kuliko hata kikosi cha Taifa Stars.
KUKOSEKANA MAKOCHA WENYE UWEZO NALO NI TATIZO LETU…
Lazima tukubali kwamba, Tanzania ina tatizo la makocha wenye uwezo wa kufundisha hasa vijana wadogo. Hata kama leo hii serikali ya Tanzania itakubali kubadili mtaala wa elimu yake na kuruhusu soka kuingia ndani yake. Tunaweza kupata tatizo la ukosefu wa makocha.
Kuna haja ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) na wadau wengine wa soka kujitolea kuwafundisha makocha wa timu za watoto ili wawe wengi watakaoweza kutoa elimu stahiki kwa watoto.
Leo hii utazunguka mitaani na kukuta watoto wanafundishwa na kocha wao, lakini ukimchungumza kocha huyo utagundua anafanya kazi hiyo kwa utashi wake tena kwa kujitolea huku akikosa elimu hata ya msingi ya ukocha. Hivi hapo unategemea kupata mchezaji bora? Hakuna.
Kozi zinazotolewa na TFF lazima zitazame hali halisi ya uwezo wa mtanzania, kwamba kozi inaletwa na kuwataka washiriki kuchangia kiasi cha fedha, basi kisiwe kingi kiasi cha kuwafanya wengine kutomudu kulipia kwani udhamini wakati mwingine unakuwa mgumu.
HITIMISHO…… NI LAZIMA TUFE ILI TUFIKE PEPONI…..!
Kwa vyovyote vile, ni lazima mambo ya msingi yafanyike katika mfumo wa soka la Tanzania ili kuiletea mafanikio nchi hii katika soka, nje hapo tutakuwa tunaimba nyimbo zisizo na muitikiaji kila siku. Mafanikio hayatakuja.
Lazima TFF na klabu za soka za Tanzania zikubali kuendesha soka kitaalam na siyo kibabaishaji kama ilivyo leo, pia ziwepo program zitakazokuwa zinafanya kazi kikamilifu na siyo zipo zipo tu kama geresha.

SOURCE:SHAFII DAUDA
-------------------

NAFASI ZA AJIRA 

JIUNGE NA AJIRA YAKO TELEGRAM GROUP HAPA

INTERNSHIP VACANCIES

GOVERNMENT VACANCIES

NGO'S VACANCIES 

GOODLUCK

Tags

Post a Comment

1 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.
  1. mtaendelea kushika mikia! acheni siyo fani yenu mna lazimishwa

    ReplyDelete

Top Post Ad