'Acheni UONGO, Nyerere Hakuwahi Kumkataa Edward Lowassa'

 AJIRA ZA UHAKIKA NJE NJE, BONYEZA HAPA

Waziri Mkuu mstaafu, Edward Lowassa, amehitimisha ziara yake ya kutafuta wadhamini katika Mkoa wa Morogoro huku kada mkongwe wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Kanali mstaafu Issack Mwisongo, akisema Baba wa Taifa hayati Mwalimu Julius Nyerere, hakuwahi kutamka kumkataa mbunge huyo wa Monduli kama ambavyo baadhi ya viongozi wanasema.

Katika Mkoa huo ambao ni wa 31, Lowassa alipata wanachama 104,038 waliomdhamini.

Kanali Mwisongo alisema tangu alipojiunga na Tanu mwaka 1967 ambayo sasa ni CCM, hajawahi kumsikia hayati Mwalimu Nyerere akitamka neno la namna hiyo na amekuwa akihudhuria vikao vyote kuanzia Halmashauri Kuu ya CCM (Nec), Kamati Kuu na Mkutano Mkuu.

“Mimi nimekuwa katika vikao hivyo vyote na kama Nyerere ukikosea au hakutaki, alikuwa anakukataa waziwazi na pia unatangazwa kwenye vyombo vya habari. Lowassa ni mtu anayewapenda Watanzania tangu zamani,” alisema Kanali Mwisongo.

Alitolea mfano wa mwekezaji aliyedai kuwa aliletwa na mmoja wa `wakubwa ' ili ajenge hoteli katika chanzo cha gesi, lakini Lowassa aliyekuwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa wakati huo, alikataa.

“Alikataza hoteli kujengwa katika chanzo cha gesi kwa manufaa ya Watanzania na kila alichoamua aliamua kwa manufaa ya Watanzania,” alisema Kanali Mwisongo.

Aidha, aliwaonya viongozi wa chama hicho kuacha kutoa matamshi kabla ya vikao havijakaa kwani ni makosa makubwa na wanasababisha CCM kuyumba kama hakina mwenyewe.

“CCM kimeyumba kupita kiasi kutokana na hawajui msemaji mkuu ni nani na vikao vikuu vinakaa saa ngapi vya kuamua hayo yanayosemwa ovyo. Viongozi wasifanye makosa katika Kamati Kuu, Kamati ya Maadili ambako kutakuwa na mizengwe, lakini watambue Nec ina nguvu,” alisema Kanali Mwisongo.

Naye Kada mwingine mkongwe, Dk. Juma Ngasongwa, ambaye amewahi kuwa Waziri katika awamu mbalimbali, alisema viongozi wa CCM wameyumba siku za karibuni kutokana na kusemana hadharani wenyewe kwa wenyewe  na Lowassa ndiye dawa ya kuondoa maneno hayo.

“Kuna wanachama wengi wamehamia vyama vingine kutokana na kushindwa kuongoza CCM. Sasa huko katika vyama vingine watawezaje kuviongoza? CCM irudishe wana-CCM imara madarakani ambaye ni Lowassa,” alisema Dk. Ngasongwa.

Kwa upande wake, aliyewahi kuwa Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Steven Mashishanga, alisema vikao vinavyotarajiwa kukaa hivi karibuni vihakikishe vinatenda haki kwa kuangalia ni nani aliye na alama nyingi za vyema mgongoni na anayehitajika na wengi.

Alisema Lowassa ni kiongozi pekee mwenye uwezo na sifa za kuwa Rais kwani amekitumikia chama kwa miaka mingi.

Naye Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Morogoro Mjini, Fikiri Juma, alimtaka Nape Nnauye, kuacha kutoa kauli kuwa wananchi wengi wamepewa fedha kwa ajili ya kumdhamini Lowassa wakati wapo wagombea wengi wamefika kuomba udhamini na kutoa rushwa.

Alisema hakuna mtu aliyepewa fedha kwa ajili ya kumdhamini Lowassa, bali ni wananchi wenyewe ndiyo wana maamuzi ya mwisho ya kumchagua kiongozi wanayemtaka na si Nape.

“Haki isipotendeka katika vikao vya maamuzi sisi bado tupo pamoja na wewe, katika semina ya wenyeviti tuliyopewa tuliambiwa tuchague viongozi wanaokubalika ndani na nje ya Chama ambaye ni wewe,” alisema Juma.

Akizungumza na wanachama CCM, Lowassa aliwashukuru kwa kumdhamini na kwamba Mkoa wa Morogoro amepata watu wengi.

Hata hivyo, alisema licha ya kupata wadhamini wengi, atapeleka wanaotakiwa CCM na wengine atawahifadhi nyumbani kwake kama kumbukumbu yake.

Lowassa amepata jumla ya wadhamini 863,479 katika mikoa 31 aliyoitembelea.

Aidha, alitaja sababu za kugombea urais kuwa ni pamoja na kuchoshwa na hali ya umaskini na pia Rais Jakaya Kikwete, anamaliza muda wake wa uongozi hivyo anatakiwa kukabidhi kijiti kwa mtu mwingine.

"Na anayeweza kukipokea kijiti hicho na kuyaendeleza yale aliyoyaacha Rais Kikwete, ni mimi. Kazi hii haipatikani hivi hivi, naomba dua zenu Waislamu na Wakristo ni muhimu sana,” alisema Lowassa.

Alisema endapo atafanikiwa kupata nafasi anayoiomba, kwanza atahakikisha anafufua viwanda katika mji wa Morogoro.

Aidha, alisema anasononeshwa mno na migogoro ya wakulima na wafugaji kwa hiyo atakapoingia madarakani, ataunda tume ya kusuluhisha migogoro hiyo.

Aliwataka Watanzania wajiandae kuwa na `spidi' ya kuchapa kazi kwani anataka mchakamchaka wa Maendeleo na  atakayeshindwa atalazimika kukaa pembeni.
-------------------

NAFASI ZA AJIRA 

JIUNGE NA AJIRA YAKO TELEGRAM GROUP HAPA

INTERNSHIP VACANCIES

GOVERNMENT VACANCIES

NGO'S VACANCIES 

GOODLUCK

Post a Comment

4 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.
  1. Nendeni mkamchague dikteta mkione cha moto si mnaowaona majirani zenu Burundi au hamna macho na masikio?

    ReplyDelete
  2. Ya Burundi waachieni wenyewe

    ReplyDelete
  3. Let's God choose. Tanzania president at the right time.

    ReplyDelete

Top Post Ad